Ads Top

AFYA ya staa wa filamu za Kibongo, Sadick Juma Kilowoko ‘Sajuki’ imetengemaa

AFYA ya staa wa filamu za Kibongo, Sadick Juma Kilowoko ‘Sajuki’ imetengemaa ambapo sasa shavu dodo baada ya kupata matibabu ya kutosha nchini India alikokwenda kutibiwa hivi karibuni, Amani limemshuhudia.
Jumatatu wiki hii, timu ya waandishi wa Global Publishers ilipiga hodi nyumbani kwa Sajuki na mkewe, Wastara Juma, Tabata-Bima jijini Dar es Salaam kwa lengo la kumjulia hali.
WASOMAJI WATAKA KUJUA HALI YA SAJUKI
Awali, baadhi ya wasomaji wa magazeti ya Global walikuwa wakipiga simu mara kwa mara kwenye chumba cha habari wakitaka kujua maendeleo ya staa huyo anayesumbuliwa na uvimbe tumboni.
Hapa tunamnukuu mmoja wa wasomaji wetu: “Jamani mmekuwa mkituandikia habari za afya ya Sajuki, tangu kuanza kuumwa, kuzidiwa, kupelekwa India na aliporudi, lakini kipindi kirefu kimepita mmekuwa kimya, vipi jamaa anaendeleaje kwani?”
MAPAPARAZI WAFUNGA SAFARI
Kufuatia sitofahamu hiyo ya wasomaji, Jumatatu ya wiki hii waandishi wetu walifunga safari hadi nyumbani kwa wawili hao.
WASTARA AKENUA MENO
Tofauti na siku za nyuma, safari hii Wastara alipowaona mapaparazi wakiingia kwake alionesha meno yote huku akiwakaribisha kwa ukarimu wa hali ya juu.
Msikilize mwenyewe: “Jamani, karibuni sana, yaani mmekuja kutujulia hali? Mungu awaongezee kwa kweli. Karibuni ndani, piteni tu, hakuna haja ya kuvua viatu.”
SAJUKI AJAA TELE KWENYE KOCHI
Tofauti na siku za nyuma alipokuwa amezidiwa, siku hiyo Sajuki alikutwa amekaa kwenye kochi akiwa amevaa ‘traksuti’ na alipowaona waandishi na yeye alitabasamu huku akisema:
“Ohooo! Karibuni sana, karibuni ndani, piteni.”
Bila kupoteza muda, Sajuki aliwaambia waandishi afya yake inavyoendelea huku akisisitiza kwamba anamshukuru sana Mungu.
“Kwa kweli jamani bila kuficha namshukuru sana Mungu, hali yangu kama mnavyoniona, naendelea vizuri sana. Nilivyo sasa si sawa na nilivyokuwa awali kabla ya kwenda India kupatiwa matibabu.
AWAKUMBUKA WATANZANIA
Sajuki aliwashukuru Watanzania waliomchangia fedha, maombi na dua akisema mambo hayo ndiyo yamechangia kwa kiasi kikubwa kuifanya afya yake ifikie ilipo sasa.
AWASHUKURU WALIOMZUSHIA KIFO
Aidha, Sajuki hakusita kuwashukuru wale wote waliotumia muda wao mwingi kutangaza kwamba yeye amefariki dunia kutokana na maradhi yake.
“Hata wale waliotumia muda wao mwingi kutangaza kwamba mimi nimefariki dunia, pia nawashukuru na Mungu awazidishie. Huenda walifanya vile kwa kuamini walichokuwa wanakifanya ni sahihi.”
WALIODAI UGONJWA WAKE NI ADHABU YA UTAPELI JE?
Sajuki alikwenda mbele zaidi kwa kusema katika maisha yake hajawahi kumtapeli mtu, lakini aliposikia kuna watu wanazusha ugonjwa wake ni adhabu kutoka kwa watu aliowatapeli alishangaa sana.
“Mimi sijawahi kumtapeli mtu, siku zote nakula kwa jasho langu. Lakini nikiwa India nilisikia eti naumwa kwa sababu niliwatapeli watu kwa hiyo waliniadhibu, nilishangaa sana! Lakini nasema hivi, hata wao nawashukuru kwa yote, Mungu awazidishie.”
WASTARA NAYE BWANA, AANGUSHA NENO ZITO
Asema: “Kuna watu wananikataza nisiseme ukweli kuhusu afya ya mume wangu eti atazidiwa zaidi, mimi nasema simuogopi mtu yeyote kwani kama ni uchawi mimi ni mchawi zaidi yao.
“Mimi naroga kutwa nzima kwa mtu mmoja tu ambaye ni Mwenyezi Mungu, lakini wao wanaroga usiku tena wakiwa na shaka hivyo sitaacha kusema mume wangu anaendelea vizuri kama hivi alivyo sasa.”
KISA CHA KUFIKA HAPA
Sajuki alianza kuugua mwaka jana ambapo alipata matibabu kwenye Hospitali ya TMJ jijini Dar es Salaam na kubainika ana uvimbe tumboni. Hata hivyo, afya yake ilizidi kwenda mrama na kusababisha kushindwa kutembea.
Wadau, mashabiki wake, ndugu jamaa na marafiki walianza ‘kampeni’ ya kumchangia fedha ili apelekwe kutibiwa nchini India ambapo Mei, 2012 alisafirishwa kwenda nchini humo na kufanyiwa upasuaji.
Sajuki alirejea nchini baada ya wiki mbili lakini hali yake ilikuwa si ya kuridhisha huku akiendelea kutumia dawa.

No comments:

UHURUTZ. Theme images by hanoded. Powered by Blogger.