Ads Top

ZANZIBA KWA CHAFUKA NA AJALI ZA MAJINI

Askari wa vikosi vya Ulinzi na Usalama wakiwa wamebeba moja ya miili ya watu waliopoteza maisha katika ajali ya boti ta Stargic iliyotokea jana karibu kabisa na Unguja.Picha na Ramadhan Othman

WATU 60 wanahofiwa kufa maji na wengine kadhaa kujeruhiwa baada ya boti iliyokuwa imebeba abiria wanaokadiriwa kufikia 250 ikitokea Dar es Salaam kwenda Unguja, Zanzibar kuzama baharini.Hii ni ajali ya pili mbaya kutokea katika kipindi cha miezi 10 tangu ilipotokea nyingine ya Meli ya Mv Spice Islander ambayo inakadiriwa kuwa watu wapatao 200 walifariki dunia.Boti hiyo iliyoondoka jana Dar es Salaam majira ya saa 6:00 mchana na kutarajiwa kufika Bandari ya Malindi, Zanzibar saa 9:30 jioni, ilizama eneo la Pungume karibu kilomita 48 kutoka Bandari ya Zanzibar.
Inaelezwa kuwa, ilianza kuzama saa 7:30 mchana kutokana na kupigwa na mawimbi mazito ya bahari.

Hata hivyo, Waziri wa Mawasiliano na Miundombinu wa Zanzibar, Hamad Masoud Hamad alithibitisha vifo vya watu 12 hadi vilivyoripotiwa ilipotimu saa 12:30 jioni jana wakati kazi ya uokoaji ikiwa inaendelea.

Baadaye saa 1:00 Ofisa Habari na Mawasiliano wa Wizara hiyo, Nafisa Madai aliwaambia waandishi wa habari kuwa idadi hiyo ilikuwa imeongezeka hadi kufikia 24 na majeruhi walikuwa 145.Madai alisema wakati boti hiyo inaondoka Dar es Salaam, ilikuwa na abiria 250 wakiwamo watoto 31 na wafanyakazi tisa.

Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Said Shaaban akizungumzia ajali ya boti hiyo ya Mv Skad, inayomilikiwa na Kampuni ya Meli Seagull alisema: “Vikosi vya uokoaji tayari vinaelekea katika eneo hilo ili kusaidia majeruhi na kufuatilia yaliyotokea.”

Maofisa kadhaa wa Serikali wakiongozwa na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Balozi Seif Ali Iddi walifika Bandari ya Malindi na Waziri wa Mawasiliano na Miundombinu Zanzibar, Hamad Masoud Hamad aliongoza msafara wa viongozi wengine kwenda katika eneo la tukio.

Awali, Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Dk Emmanuel Nchimbi alisema kuwa, hadi alipopata taarifa, watu waliokuwa wamefariki dunia ni saba na 124 ndiyo waliokuwa wameokolewa. Alisema meli hiyo ina uwezo wa kubeba abiria 300 na waliosafiri siku ya tukio hawazidi 250.

Awali, taarifa zilieleza kuwa watu 10 waliokolewa na maiti zaidi ya 60 zimenasa katika boti hiyo na kuvifanya vikosi vya uokoaji vya Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), Polisi na KMKM kupata wakati mgumu kwenye zoezi la uokoaji.Kazi ya kuokoa maisha ya watu waliozama kwenye boti hiyo na kuopoa maiti ilifanywa kwa kutumia boti nne zikiwamo za Serikali na zile zinazomilikiwa na Kampuni ya Azam Marine.
Hata hivyo, ilielezwa kwamba boti za polisi zilichelewa kwenda katika eneo la tukio kutokana na kukosekana kwa mafuta.

Akizungumza na waandishi wa habari muda mfupi baada ya kufika bandarini, Balozi Seif aliwataka wananchi kutulia na kusubiri wakiwa nyumbani wakati Serikali ikifanya juhudi za uokoaji.
Shughuli nyingi za usafiri zilivurugika kutokana na tukio hilo na Meli ya Mv Sea Bus ililazimika kufuta safari zake kupisha kazi hiyo ya uokoaji.
Mamlaka ya Udhibiti wa Usafiri wa Nchi Kavu na Majini (Sumatra), imesema inafuatilia tukio hilo kwa karibu ili kubaini chanzo.
Ofisa Uhusiano wa Sumatra, David Mziray alisema jana muda mfupi baada ya ajali hiyo kuwa, wanawasiliana na Kituo cha Utafutaji na Uokoaji Majini (MRCC), ili kupata taarifa kamili kabla ya kuujulisha umma.
Spika Makinda achafua hali ya hewa

Kutokana na ajali hiyo, muda mfupi baada ya kipindi cha jioni kuanza, Mbunge wa Wawi (CUF), Hamad Rashid Mohamed alisimama na kuomba mwongozo kwa kutumia Kanuni ya 47(3) kulitaka Bunge lipitishe Makadirio ya Matumizi ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kwa mafungu bila ya kutolewa ufafanuzi ili wabunge waweze kupata muda wa kujadili tukio hilo.
Hata hivyo, Spika Anne Makinda alipinga hoja ya Hamad na kutaka Bunge liendelee akieleza kwamba kanuni hiyo imekuwa ikitumiwa vibaya na kwamba tayari ameshawasiliana na waziri husika na kwamba taarifa kamili zitakapopatikana angelitaarifu Bunge.
Baada ya kauli hiyo Spika Makinda aliruhusu shughuli za Bunge ziendelee na kumwita Silima kutoa ufafanuzi wa hoja za wabunge.

Lakini wakati Naibu Waziri huyo akielekea kutoa hotuba yake, wabunge wote wa CUF, Chadema na baadhi wa CCM walitoka nje na kwenda katika Ukumbi wa Msekwa ili kupeana taarifa za ajali hiyo na kupanga mikakati ya jinsi ya kutuma ujumbe wa haraka kwenda Zanzibar kushirikiana na waokoaji.
Ukumbi huo uligeuka kuwa wa maombolezo kwa muda baada ya wabunge wengi kuangua vilio pale walipopewa taarifa rasmi za ajali hiyo.

Mbunge wa Wawi, Hamad Rashid alieleza kwa ufupi tukio lilivyo na kwamba wangemwomba Waziri Mkuu, Mizengo Pinda awasaidie ndege ya Serikali ili waweze kwenda Zanzibar kujumuika na wenzao katika tukio hilo.

Baada ya Hamad kumaliza alisimama Mbunge wa Kuteuliwa, James Mbatia ambaye alijaribu kuwatuliza wabunge akisema kuwa, meli inaweza kuzama lakini watu wasipoteze maisha kutokana na kuchukua muda, kauli ambayo ilipingwa na wabunge wengi.Mbunge wa Mji Mkongwe (CUF), Ibrahim Sanya alimshutumu Spika Makinda akisema, amekosa hisia na hajui kwamba kuzama kwa meli ni janga la kitaifa.
“Kwa hili hata nikikutana na Spika nitamwambia kweli ameniudhi. Sihitaji ubunge kama hali yenyewe ndiyo hii na tutapiga kura ya kutokuwa na imani na Spika,” alisema Sanya.

Wakati hayo yakitokea, katika Viwanja vya Bunge baadhi ya wabunge na mawaziri walionekana wakiwa katika vikundi wakijadili suala hilo, huku wengine wakipinga uamuzi huo wa Spika.

Wakati hayo yakiendelea katika Ukumbi wa Msekwa, Bunge lilikuwa likiendelea kumsikiliza Silima akijibu hoja za wabunge na baada ya kumaliza, Spika Makinda alimwita mtoa hoja, Waziri Nchimbi naye kujibu.Lakini badala yake, alitumia fursa yake kuondoa hoja ya Makadirio ya Matumizi ya wizara yake ili kutoa fursa kwa Bunge kujadili ushiriki wake katika tukio la kuzama kwa boti hiyo.

Dk Nchimbi alitumia Kanuni ya 58 (5) ambayo inamtaka mtoa hoja kusimama na kutoa hoja ya kuondoa mezani hoja yake kama kuna jambo la dharura.

“Mheshimiwa Spika, natumia Kanuni ya 58 (5) ambayo inamtaka Waziri kusimama na kutoa hoja ya kuondoa mezani hoja yake kama kuna jambo la dharura,” alisema Dk Nchimbi.Dk Nchimbi aliendelea: “Ikumbukwe Mheshimiwa Spika, muda mfupi kabla ya kuingia hapa ndani uliniita mimi na Naibu Waziri ukataka tukueleze hali ya ajali hiyo na kwa wakati huo Kamishna wa Matukio Zanzibar alikuwa eneo la tukio. Sasa basi, kutokana na agizo lako, ni imani yangu kwa muda aliotumia Naibu Waziri unatosha kuendelea kufuatilia jambo hilo.”

Baada ya kutoa maelezo hayo, Wabunge wote 49 waliokuwa wamebaki katika ukumbi walisimama kuunga mkono hoja.
Baada ya hapo, Spika Makinda aliwahoji na kwa kauli moja waliridhia kuahirishwa kwa kikao hicho wakati huo ikiwa saa 11:31 hadi leo saa 3.00 asubuhi, huku akiitisha kikao cha dharura cha Kamati ya Uongozi ya Bunge jana hiyohiyo kujadili suala hilo.

Akizungumza baada ya kikao hicho cha Kamati ya Uongozi, Kaimu Katibu wa Bunge, John Joel alisema, limeamua kufuta kipindi cha Maswali kwa Waziri Mkuu na kwamba kikao cha Bunge kitaendelea leo asubuhi kuanzia saa 2:00 kupokea taarifa ya Serikali kisha watajadili mustakabali wa vikao vya Bunge.Kamati hiyo pia iliamua kutuma ujumbe wa wabunge kwenda Zanzibar kuwafarijiwa wale wote walioathiriwa na ajali hiyo.

Ni ajali ya pili
Ajali Mv Spice Islander ambayo ilitokea Septemba 10, 2011 ikitokea Unguja kuelekea Pemba, ilizama kutokana na kuzidisha abiria ambao kwa mujibu wa tume iliyoundwa kuchunguza ajali hiyo, ilikuwa na abiria 2,470 na mizigo wakati uwezo wake ulikuwa kubeba abiria 600 tu.
Tume hiyo iliyoundwa na Rais wa Zanzibar, Dk Ali Mohamed Shein ilibaini kwamba ajali hiyo ilisababishwa na uzembe, kutofuata sheria na rushwa katika Bandari ya Zanzibar.

Tume hiyo ilipendekeza wahusika wa ajali hiyo kuchukuliwa hatua za kisheria na kinidhamu.
Nohodha wa meli hiyo, Said Abdallah Kinyangite, wamiliki wa meli, watendaji wa Bandari ya Zanzibar walifikishwa katika Mahakama Kuu ya Zanzibar ambako kesi zao zinaendelea.

No comments:

UHURUTZ. Theme images by hanoded. Powered by Blogger.