Ads Top

CWT: YASEMA MGOMO WA WALIMU UPO PALEPALE

Rais wa Chama cha Walimu (CWT) Gratian Mukoba akionyesha waandishi wahabari jijini Dar es Salaam jana, fomu zilizochapishwa na serikali za kuwalazimisha walimu kisaini kama wanaunga mkono mgomo au la jambo lililopingwa na chama hicho kwani ni kinyume cha utaratibu.Kushoto ni mwekahazina wa chama hicho Mohammed Utaly.Picha na Silvan Kiwale

CHAMA cha Walimu Tanzania (CWT) kimesisitiza kuwa, mgomo wake uliopangwa kuanza leo upo palepale.
Hatua hiyo ya CWT imekuja siku  moja baada ya Serikali kutangaza kuwa mgomo huo ni batili.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana, Rais wa CWT, Gratian Mukoba ameitaka Serikali kuacha vitisho dhidi ya walimu.
Alisema kuwa Serikali imekuwa ikiwalazimisha walimu kujaza fomu zinazowataka kuorodhesha majina yao na shule wanazofundisha na kueleza kama wanaunga mkono mgomo huo au la.CWT imesema walimu wanatakiwa kushiriki mgomo huo kwa kuwa ni halali na umeitishwa na chama hicho kwa kufuata taratibu zinazotakiwa.
Mukoba alisema, Baraza la CWT lilitoa notisi ya saa 48 kuanzia jana (juzi) saa 8 mchana, ambayo inamalizika leo saa 8 mchana, kisha kutangaza rasmi kuwa utekelezaji wa azma yao ya kugoma unaanza kesho.
“Walimu wataanza mgomo rasmi Jumatatu (kesho), kwa kubaki nyumbani bila ya kwenda kazini hadi watakapotaarifiwa vinginevyo na Rais wa CWT,” alisema Mukoba.
Alisema kuwa, wanachama waliopiga kura kuamua kuwepo kwa mgomo walikuwa 183,000  ambapo kati yao 153,000  waliunga mkono azimio hilo wakiwa sawa na asilimia 95.7 ya wanachama, hivyo kuhalalisha mgomo huo.
Hata hivyo, Mkoba alisema kuwa  mgomo huo hautahusiana na zoezi la Sensa ya Watu na Makazi litakalofanyika Agosti 26, mwaka huu ambapo aliwataka walimu kushiriki kikamilifu.
“Walimu wanahakikishiwa kuwa mgomo hautaathiri utumishi wao kwa kuwa umezingatia sheria, ingawa tunategemea kuwapo kwa vitisho na propaganda nyingi kutoka kwa waajiri wetu,” alisema Mukoba.Mukoba alieleza kuwa mgogoro uliotangazwa na walimu kupitia CWT ulishindikana kusuluhishwa na msuluhishi aliyeteuliwa na Tume ya Usuluhishi na Uamuzi (CMA).
"Nawataka walimu wote nchini kuungana  na kuhakikisha  kuwa mnashiriki zoezi hili lenye lengo la kumshinikiza mwajiri wetu (Serikali) kusikiliza madai yetu," alisema.
Alhamisi wiki hii CWT ilitangaza mgomo wa walimu nchi nzima kupinga Serikali kushindwa kuwatimizia madai yao ya siku nyingi ikiwamo ongezeko la mishahara.
Madai ya walimu
Madai ambayo walimu wamekuwa wakiitaka Serikali kuyatafutia ufumbuzi ni pamoja na ongezeko la mishahara kwa asilimia 100, posho ya kufundishia kwa walimu wa Sayansi asilimia 55, asilimia 50 kwa walimu wa masomo ya  sanaa na posho kwa  walimu wanaoishi katika mazingira magumu.Mgogoro kati ya CWT na Serikali umedumu kwa zaidi ya miaka mitano sasa, ambapo licha ya ahadi ya kulipwa madai hayo, fedha zimekuwa hazikidhi ukubwa wa tatizo na kusababisha madeni kurundikana.
Hata hivyo, Serikali juzi ilitoa taarifa kwa vyombo vya habari iliyosainiwa na Kaimu Katibu Mkuu Kiongozi, Paniel Lyimo ikieleza kuwa walipokea notisi  kutoka CWT kuwataarifu juu ya mgomo utakaofanyika kesho nchi nzima.
“Kabla ya notisi hii kutolewa, Serikali imekuwa ikifanya jitihada nyingi za kujadili na viongozi wa CWT kuhusu jinsi ya kuboresha masilahi ya walimu kwa nia ya kumaliza suala kwa maelewano kwa kutumia vyombo na ngazi mbalimbali,” ilieleza sehemu ya taarifa hiyo.
Taarifa hiyo ilieleza kuwa shauri hilo liko Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi na kwamba juzi mchana pande zote mbili zilifika Mahakamani na Mahakama ikaamuru pande zote zikamilishe maelezo yao ifikapo Jumanne.
Kauli ya WizaraNaibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Philipo Mulugo alipoulizwa jana kuhusu uamuzi wa walimu kuendelea na mgomo, alisema hawezi kuzungumzia hilo yuko safarini kuelekea Mbeya.
“Siwezi kuzungumza nipo safarini kuelekea Mbeya na hatuwezi kuelewana hivyo,  mtafute Waziri atazungumzia,” alisema Mulugo.
Hata hivyo, Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi, Dk Shukuru Kawambwa alipopigiwa simu yake ya mkononi iliita bila ya kupokewa.
Walimu Bunda Kutoka Bunda, Ahmed Makongo anaripoti kuwa  siku moja baada ya CWT, kutangaza mgomo wa walimu usiokuwa.

Mwenyekiti wa chama hicho wilayani Bunda, Francis Ruhumbika aliwataka walimu wote wilayani humo kushiriki kwenye mgomo huo bila kwenda kwenye vituo vyao vya kazi, baada ya notisi ya masaa 48 kumalizika.
Akizungumza na mjini Bunda jana, Ruhumbika pia amewataka walimu wote wilayani humo, kutokukubali kusaini fomu yoyote itakayoletwa na viongozi wa Serikali, itakayowataka walimu wanaounga mkono au wasioutaka mgomo kusaini fomu hiyo.

Arusha Kutoka Arusha Peter Saramba, anaripoti kuwa CWT  Wilaya za Arumeru na Manispaa ya Arushawametangaza kuunga mkono tamko la mgomo usio na mwisho uliotangazwa na Baraza Kuu la Taifa la chama hicho.Wakitoa tamko mbele ya waandishi wa habari katika Ofisi za CWT Mkoa wa Arusha jana, Mwenyekiti wa CWT Wilaya ya Arumeru, Elifas Ole Saitabauna Martin Godfray kutoka Manispaa ya Arusha walisema hakuna njia nyingine ya kusimamisha mgomo huo isipokuwa Serikali kutekeleza madai yao. “Sisi ngazi ya wilaya na mkoa tunaunga mkono mgomo huo na tunawataka walimu wasiogope vitisho, atakayetishiwa atoe taarifa mara moja kwa uongozi wa eneo lake,” alisema Ole Saitabau.

No comments:

UHURUTZ. Theme images by hanoded. Powered by Blogger.