Ads Top

Umeme wasitisha kikao Baraza la Wawakilishi

 
 Baraza la Wawakilishi 

KIKAO cha Baraza la Wawakilishi kinachoendelea Chukwani Unguja, kimelazimika kusitishwa kwa muda kutokana na hitilafu ya umeme iliyotokea katika ukumbi wa baraza hilo la wawakilishijana asubuhi.

Akitoa tangazo kwa wajumbe wa baraza hilo, Spika Pandu Ameir Kificho aliwaambia wajumbe kwamba kutokana na hitilafu hiyo kikao hicho anakiahirisha hadi jioni ili kutoa fursa kwa mafundi wa umeme kuja kufanya matengenezo katika ukumbi huo.

Spika Kificho alisema licha ya kuwashwa jenereta na kuendelea na shughuli za baraza hilo, lakini kutokana na ukubwa na mahitaji makubwa ya umeme katika ukumbi huo, majenereta hayo hayana uwezo wa kumaliza shughuli nzima ya vikao vya baraza hilo na hivyo wanalazimika kuwapisha mafundi kuendelea na kazi ya matengenezo.

“Waheshimiwa wajumbe kutokana na hitilafu ya umeme katika ukumbi wetu huu, naomba kuahirisha kikao hiki hadi hapo jioni, ili tutoe nafasi kwa mafundi waliofika hapa kuja kututengenezea umeme kwa sababu jenereta lililowashwa haliwezi kutumalizia shughuli yetu hii muhimu” alisema Spika.

Hata hivyo wajumbe wa baraza la wawakilishi walionekana kutoka wakiwa na furaha baada ya kusikia kikao hicho kimeahirishwa na waliendelea jioni baada ya matengenezo hayo kufanywa na wataalamu na mafundi kutoka Shirika la Umeme la Zanzibar (Zeco).

Ukumbi wa baraza la wawakilishi umejengwa kwa ufadhili wa Sheikh Ali Yussuf wa Saudi Arabia na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, lakini ukumbi huo umekuwa na hitilafu za mara kwa mara katika mitambo yake ya umeme, vipaza sauti na hata baadhi ya sehemu ya jengo hilo limekuwa likivuja.

Ofisa mmoja wa baraza hilo aliliambia gazeti hili kwamba ujenzi wa jengo hilo haukuwa mzuri katika ramani yake kutokana na kuwa mafundi wa Mamlaka ya Maji Zanzibar (Zawa) wameshindwa kuona njia na paipu za kupitishia maji machafu na hivyo kuvuja kwa maji kumeshindikana licha ya juhudi kadhaa kufanywa na wataalamu wa Zawa kujaribu kutaka kufanya marekebisho njia hizo za maji ndani ya jengo hilo.

“Jengo hili tokea limejengwa kuna matatizo mengi si unakumbuka wawakilishi wakilalamikia vipaza sauti havisikiki na sasa umeme una matatizo, pia kuna tatizo la maji hapa wamekuja mafundi na wataalamu wengi sana, lakini wameshindwa kuona paipu hawajui zimefukiwa au zimezamishwa wapi kwa hivyo maji yanamwagika na hayana pa kutokea na wale waliojenga wala hawapo sasa sijui tena serikali itafanyaje,” alisema.

No comments:

UHURUTZ. Theme images by hanoded. Powered by Blogger.