Njaa: Wananchi washindia uji, mchicha pori
TATIZO la upungufu wa chakula limeyakumba maeneo mengi nchini na sasa kuna baadhi ya maeneo wananchi wameanza kula mizizi.
Uchunguzi
uliofanywa na Mwananchi unaonyesha kuwa baadhi ya maeneo yaliyoathirika
kwa njaa kuwa ni pamoja na Wilaya ya Ngorongoro, mkoani Arusha, Handeni
na Kilindi mkoani Tanga, Nkasi mkoani Rukwa na baadhi ya maeneo ya Mkoa
wa Shinyanga.
Wilayani Ngorongoro hali ni mbaya zaidi katika Tarafa
ya Ngorongoro, ambako idadi kubwa ya watu wa eneo hilo, wanaishi kwa
kula matunda na mchicha wa porini.
Tarafa hiyo iliyopo ndani ya eneo
la Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro, ina wakazi wanaofikia 70,000, ambao
ni wafugaji wa jamii ya Kimasai waliohamishiwa kwenye eneo hilo kutoka
Hifadhi ya Taifa ya Serengeti wakati ilipoanzishwa.
Eneo hilo lenye
njaa ni moja ya maeneo maarufu duniani yaliyotangazwa na Shirika la
Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO) kuwa ni eneo la
urithi wa dunia.
Kwa sasa eneo hilo, linaingiza kiasi cha Sh52
bilioni kwa mwaka, ikiwa ni mapato yanayotokana na watalii wanaoingia
kwenye hifadhi.
Kinachowavutia watalii kutembelea eneo hilo, pamoja
na vivutio vingine vya utalii ni kuangalia maisha ya watu wa jamii ya
Kimasai wanavyoishi pamoja na wanyamapori kwenye kasoko (shimo la
volcano).
Hali ya njaa kwa sasa
Pamoja na kuwa eneo hilo
linakabiliwa na njaa, kumekuwapo na mvutano baina ya baadhi ya viongozi
wa Mkoa wa Arusha, Wilaya ya Ngorongoro pamoja na Mashirika yasiyo ya
Kiserikali (NGO’s) juu ya ukweli kuwapo kwa njaa.
Kila upande umekuwa na tamko lake kuhusiana na tatizo la njaa Ngorongoro.
Wakati
Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Magesa Mulongo akisema eneo hilo, linakabiliwa
na upungufu wa chakula, Mbunge wa Jimbo la Ngorongoro, Saning’o Ole
Telele pamoja na NGO’s wanasema eneo hilo lina njaa kali.
Hata hivyo,
Mwananchi hivi karibuni ilitembelea vijiji vya Kata za Nainokanoka,
Enduleni, Alailelai na Kata ya Ngorongoro na kushuhudia watu wengi
katika wilaya hiyo wakikabiliwa na njaa.
Kijana mlinzi wa miaka 18 analea familia ya watu 16.
Moja
ya familia, ambayo inakabiliwa na njaa katika eneo hilo ni ya kijana
Menguru Parisani (18), yenye watu 16, wengi wakiwa wanawake na watoto.
Hata hivyo, Perisani mwenyewe amelazimika kwenda jijini Mwanza kufanya kazi ya ulinzi, ili apate fedha za kulisha familia.
Baada
ya kufika nyumbani kwa Perisani, mwandishi wa habari hizi alikutana na
wanawake wawili, waliokuwa wakijiandaa kwenda kusaga wastani wa kilo
tano za mahindi.
Nahoro Ngidadya ni mama wa watoto wanne katika
familia hiyo, aliyejitambulisha kuwa ni mjane, ambaye mumewe alifariki
katika ajali ya gari, hivi karibuni akiwa anafanya kazi ya kibarua.
Anaeleza
kuwa mwanamume huyo, alipofariki alimwacha na ng’ombe mmoja ambaye
ndiye wamekuwa wakimtegemea kwa kupata maziwa wanayokunywa.
Huku akionekana kukata tamaa, anasimulia kuwa maisha yake ya kila siku na watoto wake yamekuwa magumu.
“Watoto
wangu Nasabuko, Chinene bado ni wanafunzi, Oturohu na Laitelei
hawajaanza masomo wakiamka asubuhi nimekuwa nikiwapa chai ya maziwa
isiyo na kitafunwa, wanakwenda shule na wakirudi mchana nawakorogea uji,
wanaokunywa pamoja na kuwachemshia mchicha pori au mnafu,” anasimulia
mama huyo.
Huku akionyesha mboga hizo, zinazopatikana katika mapori
ndani ya tarafa hiyo, Ndidadya anasema kuwa kwa zaidi ya wiki mbili
sasa, amekuwa akiwapa watoto uji na mboga hizo.
“Kuna wakati watoto
hawa hukosa nguvu na hupata kizunguzungu, lakini sina cha kuwapa zaidi
ya uji, kwani siwezi kutumia unga kidogo nilionao kuwasongea ugali,”
anasema Ndidadya.
Mwandishi alishuhudia watoto wa familia hiyo
wakirejea kutoka shuleni mchana wakiwa wamechoka, huku wazazi wao
wakisubiri kusaga mahindi kabla ya kurejea na kuwakorogea uji.
Naye
Noondomono Parsani anayetoka katika familia hiyo, akiwa na watoto
watatu, awali anakataa kuzungumza akieleza haelewi lugha ya Kiswahili
lakini anajitokeza mkalimani na kutuwezesha kuwasiliana.
Parsani
anaeleza kuwa maisha yao ni duni na kila siku hawajui kesho yao
itakuwaje na kwamba licha ya kupewa mahindi ya msaada, debe moja
limeshindwa kusaidia familia yao.
“Sasa wanakupa debe moja kwa miezi miwili, utakulaje? Ni bora tu kupika uji kwani ugali unatumia unga mwingi,”anasema Parsani
Anasema
kuwa ingawa kwa sasa kuna mahindi yanayouzwa Sh9,000 kwa debe, lakini
familia yao haina uwezo wa kununua, kwa kukosa fedha, wala ng’ombe wa
kukamua ili wauze.
“Hata kama tungekuwa na ng’ombe wa kutosha kukamua
maziwa, sasa huku utamuuzia nani maziwa. Kikubwa, huku tupate chakula
tu, kwani kilimo kimezuiwa,” anasema Parsani.
Kutokana na hali ya
familia hiyo, mwandishi alilazimika kuisaidia familia hiyo kwa kuipa
fedha kidogo ili wanunue mahindi na baadaye kwenda katika familia
nyingine.
Lita moja ya maziwa yaokoa maisha ya wajukuu.
Katika
familia nyingine eneo la Nainokanoka, mwandishi alikutana na Naromay
Lembirika aliye na umri unaofikia miaka 65, akiwa amekaa barabarani na
kidumu kidogo cha lita moja ya maziwa.
Baada ya kumuuliza alisema
kuwa anauza maziwa hayo, Sh500 kwa lita moja, lakini amekaa njiani hapo
kwa zaidi ya saa tatu, bila kupata mteja.
kwa habari zaidi bofya hapa..>>>
kwa habari zaidi bofya hapa..>>>
No comments: