Ads Top

Papa Benedict aahidi utii kwa ajaye

Papa Mstaafu Benedict wa kumi na sita
 
 HUKU  mchakato wa kumpata papa mpya ambaye ataongoza Kanisa Katoliki ukianza Jumatatu Machi 4, mwaka huu, Papa Mstaafu Benedict XVI ameaga akiahidi utii kwa mrithi wake.
Katika salamu zake kwa makardinali jana, muda mfupi kabla ya kung’atuka rasmi, Papa Benedict alieleza kuwa atakuwa karibu na mrithi wake bila migongano.

Kauli hiyo imetolewa wakati kukiwa na hofu miongoni mwa walei, watawa kwamba huenda viongozi hao wakaingia katika mzozo wa madaraka.

Hata hivyo, wakati akitoa ahadi hiyo, mchakato huo unaanza  huku ajenda muhimu zikiwa ni jinsi ya kulisafisha kanisa hilo ambalo limekumbwa na kashfa kadhaa.

Kashfa hizo ndizo zinazotazamiwa kutawala kikao cha makardinali kinachoanza Jumatatu.

Ingawa ni makardinali 115 kati ya 117 wenye sifa ya kupiga kura ya kumpata papa mpya,tayari makardinali  wengi akiwamo Kardinali Polycarp Pengo kutoka Tanzania wapo Vatican kushuhudia kazi hiyo ngumu.

Ni kazi ambayo inaweza kuchukua hadi wiki tatu ikiongozwa zaidi na sala, mafungo huku wapigakura ambao ni makardinali wenye umri chini  ya miaka 80 wakikabiliwa na changamoto lukuki.

Kwanza, ni azma ya wengi ya kulisafisha kanisa hilo kubwa duniani linalokabiliwa na tuhuma nyingi zikiwamo za baadhi ya viongozi wake kuwadhalilisha watoto kijinsia, kuvuja kwa nyaraka za siri kutoka ofisi ya Papa Benedict XVI ambaye amestaafu.

Nyingine ni ufisadi katika benki inayomilikiwa na kanisa hilo iliyo sababisha uongozi wake kuondolewa  mwaka jana na maofisa wake kushtakiwa.

Awali, Papa Benedict Jumatano aliwaaga maelfu ya waumini, watawa ambaye jana aliondolewa Vatican usiku wa saa 2.00 (saa 4:00 za usiku kwa Tanzania) kwa helikopta maalumu ili kuanza maisha mapya katika makazi ya papa, majira ya kiangazi, Castel Gandolfo, kusini mwa Rome.

Ulinzi wake kwa sasa utakuwa chini ya polisi wa kawaida badala ya walinzi wake raia wa Uswisi ambao kibarua chao kilimalizika rasmi jana usiku.

Lakini, nyuma yake kiongozi huyo ameacha waumini bilioni 1.2 huku baadhi ya maeneo mengine kama Ulaya na Marekani, watumishi hasa mapadri na watawa wakiwa wamepungua.
Sababu hiyo inalifanya Bara la Afrika kuonekana kuwa eneo linalokua kiimani lenye waumini 177 milioni na kusababisha bara hilo kupigiwa upatu kwamba linaweza kutoa mrithi wa Papa Benedict.
Makardinali, Peter Turkson kutoka Ghana na Francis Arinze wa Nigeria,mwenye umri zaidi ya miaka 80, wanatajwa kuwa miongoni mwa wanaofaa kwa kazi hiyo.
Katika hotuba yake Jumatano, Papa Benedict alieleza kuwa maisha  yake Vatican yalikuwa yenye furaha, huzuni baada ya kupitia vipindi vigumu na wakati mwingine rahisi.
"Kuna kipindi ambako bahari ilichafuka, mawimbi na pepo zilivuma dhidi yetu ... wakati mwingine Mungu alielekea kuwa amelala."
Kuhusu sifa ambayo makardinali hao wangependa awe nayo mrithi wa Papa Benedict XVI, wapo wanaodhani kuwa hakutakuwa na mabadiliko makubwa kwani viongozi wa kanisa hilo ni watu wasiopenda mabadiliko.
Kwa maana hiyo, makardinali wachache  watapenda kuona mabadiliko ndani ya kanisa hilo.
Kwa mtazamo wa wengi, mfumo utawazuia wengi kukimbilia mabadiliko na kitu ambacho watakitafuta makardinali ni kupata mtandao mkuu miongoni mwao.
Pia, wapo wengine ambao wanafikiri kuwa makardinali wangependa kumpata mtu ambaye ni mzungumzaji mzuri.  Lakini, hawalazimiki kumteua mtu anayezungumza lugha nane kama za Papa Benedict na mtangulizi wake, Mwenyeheri Yohani Paul II, ila kiongozi  anayefaa kuingia madarakani  na kutambulika kuwapo kwake duniani.  
Sifa nyingine ambayo inatazamiwa kuangaliwa ni ya kiongozi ambaye atakuwa mtu wa watu, tofauti na  Papa Benedict XVI ambaye alishindwa kufuata nyayo za Mwenyeheri Yohane Paul  II.Kwa wengine ndani ya kanisa, Papa  Benedict  XVI anaonekana kuwa alishindwa kuwafikia wengi, yakiwamo makundi ya watu ambao walikuwa tayari kumsikiliza.
Wakosoaji wa mfumo wa kumpata papa mpya wanaeleza kuwa suala la makardinali kutozungumza wakati wote wa mchakato unazuia mijadala kuhusu hali ya baadaye na ustawi wa kanisa, hasa kwa kuzingatia ukweli kwamba kanisa hilo linaonekana kuwa limefungwa.
Kuondoka kwa papa madarakani baada ya miaka 600 iliyopita kunaelekea kuwa kumeacha ombwe, mtazamo ambao unaungwa mkono na mwanahabari mwandamizi wa Vatican, John Thavis.
Thavis anaeleza kuwa  watu wengi waliopo Vatican hawana mpangilio wa kazi zao, wamechanganyikiwa kutokana na kung'atuka  ghafla kwa papa.
Kwa mtazamo wa wengi, uamuzi wa papa kung'atuka ulikuwa wa dharura mno, kiasi kwamba hakuwahusisha wengine, jambo ambalo linalifanya ofisi yake iliyoko  Vatican pamoja na  wasaidizi wake kuwa na wakati mgumu kusaka majibu.
"Kila mmoja anataka kuandika historia, lakini hakuna anayejua lipi litatokea baadaye.
"Kuna  tatizo la kutoa maamuzi Vatican, utaratibu umebakia  zaidi wa kimila. Ni uamuzi ambao unategemea zaidi watu binafsi, bila kuangalia mtazamo wa jamii," anaeleza Thavis.
Mwandishi huyo ambaye ameishi na kufanya kazi katika Shirika la Habari la Catholic News Services kwa miaka 30 anaamini kuwa kumekuwa na wakati ambao papa alikatishwa tamaa na alitambua hilo.
Pia, alifikia mahali pa kuona amesalitiwa, anaeleza mwandishi huyo katika kitabu chake, Vatican Diaries na kuongeza kuwa hilo lilimuumiza binafsi papa, ambaye hata hivyo aliumia kila alipokosolewa.
Jambo lingine ambalo limeachwa na papa huyo aliyestaafu ni kukosekana kwa uwazi katika baadhi ya mambo yakiwamo ya utoaji zabuni, mambo ambayo yanaweza kuitwa kuwa ni rushwa ndogo zilizotendeka Vatican.

No comments:

UHURUTZ. Theme images by hanoded. Powered by Blogger.