SALAMU ZA BODI YA FILAMU TANZANIA KATIKA MSIBA WA GEORGE OTIENO OKUMU
Katibu Bodi ya Filamu Bibi Joyce Fisoo akisoma salamu za rambirambi
wakati wa kuuaga mwili wa aliyekua mtayarishaji wa filamu nchini George Otieno
Okumu “Tyson” katika viwanja vya Leaders’ Kinondoni. Tyson alifariki mwishoni
mwa wiki iliyopita kwa ajali ya gari.
Ndugu
zangu nashindwa hata niseme nini kutokana na mfululizo wa misiba ya wanatasnia
wenzetu, nashindwa kueleza simanzi kubwa niliyonayo, nakosa la kuongea ninabaki
kusema kazi ya Mungu haina makosa katika yeye tumeubwa na yote yanayotokea ni
kwa mapenzi yake yeye aliye muumba.
Bodi
ya Filamu nchini inaungana na wadau wote wa filamu pamoja na familia kufuatia
kifo cha ghafla cha mwongozaji mahiri wa filamu ndugu yetu George Otieno Okumu
(Tyson) kilichotokea kwa ajali ya gari. Ninatambua wakati mgumu ambao familia
yake unao, watoto wake, wanatasnia wote na wafanyakazi wenzake wa TV 1.
Jina
George Tyson lipo masikioni mwa watanzania tangu mwanzoni mwa mwaka 2000 na limetambulishwa
na umahiri wa kazi alizoziongoza ikiwemo filamu iliyoitwa Girl friend ambayo ilitikisa soko la filamu. Tyson ni miongoni mwa
wanatasnia waliotoa mchango mkubwa katika kuinua tasnia ya filamu hapa nchini
na katika kuongoza vipindi mbalimbali vya runinga.
Nyote
mnakumbuka kundi la Mambo Hayo ambalo ndugu yetu Tyson alikuwa mmoja wa waasisi
wakubwa. Wanatasnia wengi walio mahiri hapa nchini wamebahatika kupata fursa ya
kufundishwa na Tyson.
Tyson
ameweza kutambulisha na kukuza vipaji vingi, kimsingi aliwekeza katika kufundisha
makundi mbalimbali ya wanatasnia, alikua mahiri na kwa hakika amechangia katika
kukua na kuendeleza tasnia ya filamu nchini.
Ni
ukweli usiopingika kuwa msisimko mkubwa miongoni mwa wafanyakazi wa tasnia ya
filamu nchini uliongezwa na kazi alizofanya ndugu yetu Tyson. Kuondoka kwake ni
pigo kubwa sana kwetu wanatasnia. Daima tutamkumbuka kwa mchango wake, katika
kuendeleza juhudi zake nawasihi wanatasnia tuenzi yale yote mema aliyotuachia
na tuyaendeleze.
Narudia
kutoa pole nyingi na Mungu atupe subira katika kipindi hiki kigumu cha
maombolezo.
Daima
tumkumbuke na kumuenzi.
MUNGU
AILAZE ROHO YA MAREHEMU GEORGE OTIENO OKUMU (TYSON) MAHALI PEMA PEPONI AMENI.
No comments: