Mvua kubwa iliyonyesha jana jijini Dar es Salaam, ilisababisha mafuriko makubwa katika baadhi ya maeneo
Mvua kubwa iliyonyesha jana jijini Dar es Salaam, ilisababisha
mafuriko makubwa katika baadhi ya maeneo, hivyo nyumba kadhaa kujaa maji
na baadhi ya watu kulazimika kuyahama makazi yao.
Mafuriko hayo yaliyosababishwa na mvua iliyoanza
kunyesha muda wa asubuhi, pia yalisababisha hasara kubwa kutokana na
vitu na mali mbalimbali kusombwa na maji.
Mwananchi lilitembelea maeneo mbalimbali na
kushuhudia wananchi wakihangaika kuokoa mali zao, baada ya nyumba
walizokuwa wakiishi kujaa maji.
Barabara kadhaa zilikuwa hazipitiki kutokana na
kujaa maji, huku baadhi ya nguzo za umeme na simu ambazo zilikuwa karibu
na mifereji ziliharibiwa na kusombwa na maji.
Mafundi wa Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco)
walionekana katika maeneo kadhaa ya jiji wakihangaika kuokoa baadhi ya
nguzo hizo.
Athari kubwa ya mafuriko hayo ilitokea katika eneo
la Kigogo Darajani ambako baadhi ya nyumba zilikuwa zimejaa maji na
baadhi ya vitu vilionekana vikielea kwenye mikondo mikubwa ya maji.
Mmoja wa waathirika hao, Andrew Simon (35) alisema
nyumba yake ilijaa maji kwa takriban futi nne kwenda juu na kusababisha
hasara ya mali ambayo alikuwa bado hajafahamu thamani yake.
“Sisi tulitoka kwenda kwenye shughuli zetu,
baadaye tulipigiwa simu kwamba kuna mafuriko jambo lililonifanya nirudi
haraka ndiyo nikakuta nyumba yetu ikiwa imefurika, huku vyombo vyote
vikiwa vimeharibika,” alisema Simon.
Kuhusu kutii agizo la Serikali la kuwataka
wananchi wa mabondeni kuyahama makazi yao, Simon alisema yeye ni
mpangaji hakufahamu kuwa mafuriko yangetokea.
Mbali na Kigogo Darajani maeneo mengine ya Ubungo,
Tabata, Magomeni Kagera, Jangwani, Msasani, Mikocheni, Kimara na Mbezi
pia yaliathiriwa na mvua hizo hali iliyozua hofu miongoni mwa wakazi wa
maeneo hayo.
Pia hali ilikuwa mbaya eneo la Tabata Relini
nyumba na magari vilifunikwa na maji na kuwafanya watu kupanda kwenye
mapaa ya nyumba zao.
Reli inayopita katika eneo hilo ilifunikwa na maji
kiasi cha kusababisha kuwapo kwa wasiwasi kama treni ya usafiri wa
abiria itafanya kazi leo.
Eneo jingine lililoathirika ni lile la Ubungo-Maziwa, karibu na
Daraja la External ambalo ujenzi wake unaendelea ambapo Meneja Masoko wa
Kampuni ya Mwananchi Communications Limited, Bernard Mukasa alikuwa
miongoni mwa watu walioathirika na hali hiyo.
Mukasa alisema kuwa mafuriko hayo yalisababishwa
na kuzibwa kwa mifereji kutokana na kazi ya ujenzi wa barabara
inayoendelea katika eneo hilo.
“Tulishalalamika siku nyingi kuwa hawa wajenzi wa
barabara wanaziba mifereji wakati wa kazi zao na wangetusababishia
madhara mvua ikinyesha, lakini hakuna kilichofanyika”alisema Mukasa, .
Mwaka jana wakazi wa Jangwani walikumbwa na
mafuriko kama hayo, walihamishiwa katika eneo la Mabwepande ambako
walipewa viwanja kwa ajili ya ujenzi wa makazi ya kudumu. Licha ya hatua
hiyo, baadhi ya wakazi hao bado wanaendelea kuishi katika eneo hilo
hadi sasa.
Makamanda wanena
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Temeke, Englebert Kiondo
alisema :“Mpaka sasa sijapokea taarifa yoyote ya matukio kuhusu mvua
inayoendelea, ila wasaidizi wangu wameniambia maeneo yote yapo salama
hakuna mafuriko wala maafa kama kukiwa na taarifa zaidi ya hizi
nitakutaarifu”.
Naye Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Kinondoni,
Charles Kenyela alisema mvua hiyo imesababisha adha kubwa katika mkoa wa
wake kutokana na baadhi ya barabara kujaa maji na kushindwa kupitika
ikiwamo ya Mwai Kibaki.
Kamanda Kenyela alisema katika barabara hiyo
baadhi ya abiria walipata shida ya usafiri kwani maji yalikuwa yamejaa
juu ya barabara hiyo.
Alisema Daraja la Mbezi pia lilijaa maji
kusababisha watumiaji wa njia hiyo kuhangaika kuvuka. “Hakuna binadamu
aliyepoteza maisha kutokana na mvua hiyo, ila baadhi ya barabara zimejaa
maji na kuleta kero kwa watumiaji,” alisema Kamanda Kenyela.
Alisema baadhi ya nyumba eneo la Manzese zilijaa
maji na kusababisha usumbufu mkubwa kwa wananchi, huku baadhi ya
barabara zilizojaa maji zikishindwa kupitika hivyo kusababisha foleni ya
magari na usumbufu kwa watumiaji wengine.
Alipotafutwa Kamanda wa Mkoa wa Kipolisi wa Ilala, Marietha Minangi hakuweza kuongea kwa kuwa alidai yupo kwenye mkutano.
Habari hii imeandikwa na Nuzulack Dausen, Bakari Kiango na Suzan Mwillo.
No comments: