Ads Top

NAMNA MWANAMKE ANAVYOWEZA KUTUMIA NAFASI ZAKE KUBADILISHA MAISHA YA NDOA YAKE



Kila mwanamke aliye na hekima huijenga nyumba yake: Bali aliye mpumbavu huibomoa kwa mikono yake mwenyewe’. Tafsiri ya neno nyumba ni familia, naam na familia inajumuisha baba, mama na watoto endapo mmejaliwa. Hata hivyo katika hali ya kawaida watoto watalelewa katika msingi mzuri endapo ndoa husika imetengamaa. Ifahamike kwamba hili andiko si la wanandoa peke yao, bali hata wanawake wasio wanandoa wenye familia kama wajane, walezi nk linawahusu. Kwa kuwa hapa tunazungumzia habari za wanandoa nitalifafanua zaidi kutoka kwenye kona hiyo. Pia neno nyumba limetumika ili kutupatia urahisi wa kuelewa namna nyumba za kawaida zinavyojengwa ili tueguze dhana hiyo kiroho pia. Kwa lugha rahisi ndoa yako ni nyumba, hivyo ubora, uzuri na mvuto wa ndoa yako unategemea namna unavyoijenga daima kwa hekima.
Ni vizuri ukafahamu kwamba suala la ujenzi/maboresho ya ndoa yako ni jukumu la kila siku ya kuishi kwa ndoa yenu mpaka kifo kiwatenganishe. Kila mmoja katika ndoa ni lazima ahakikishe anasimama kwenye nafasi yake na kufanya yale yampasayo ili kuifanya ndoa yake kuwa bora zaidi. Endapo hakutakuwa na jitihada za wanandoa katika kuimarisha ndoa yao, Shetani atatumia fursa hiyo kuivuruga ndoa husika. Kujenga kunakozungumziwa hapa ni kule kuhakikisha ndani ya ndoa kuna mahusiano na mawasiliano mazuri baina yenu ambayo yatafanikisha kutekelezwa kwa kusudi la Mungu.
Ukweli wa ajabu na wa pekee
Ni ajabu sana kuona kwamba jukumu la ujenzi wa ndoa/nyumba amepewa mwanamke. Hii haina maana mwanaume hahusiki, hapana, bali ki-nafasi jukumu la ujenzi wa nyumba/ndoa ni la kwako mama. Kumbuka nilikueleza kwamba nafasi hizi tano za Mwanamke katika ndoa zinafanya kazi kwa pamoja na kwa kutegemeana. Katika nafasi hii ya ujenzi unapaswa kuhakikisha unajenga ndoa yako ili kuzuia kila ufa/fursa ambayo Shetani anaweza kutumia kuvuruga ndoa yako. Kumbuka katika hali ya kawaida kujenga ni kuimarisha/kuweka mazingira bora juu ya kile unachokithamini ili kuzuia madhara yanayoweza kutokea. Naam nafasi hii inalenga kukusaidia uwe makini sana na kila kinachoweza kubomoa ndoa yake.
7
Suala la ujenzi wa ndoa ni endelevu kwa sababu siku zote adui anatafuta kubomoa ndoa yako. Ni lazima uwe makini kujua wapi ni mahali palipobomoka ambapo Shetani anapatumia sasa kuharibu ndoa yako au anaweza kutumia baadaye kuharibu ndoa yako, naam ukishajua kwa kutumia hekima, jenga ukuta imara ambao adui hawezi penya. Kama ndoa yako ina nyufa basi ni rahisi adui kupita kwenye hizo nyufa. Kumbuka hata  kama umemaliza kujenga kila kitu kwenye nyumba yako, bado kuna matengenezo ya mara kwa mara yanahitajika ili kuifanya nyumba yako kudumu katika hadhi inayostahili. 
Maeneo ya msingi katika kujenga ndoa yako
  • Utiifu kwa mumeo
Maandiko yanasisitiza sana wanawake kuwatii waume zao (Waefeso 5:22-24,                1 Petro 3:1). Mitume walindika maandiko haya ili kuwaonya wanawake kutokana na mienendo yao mbele za waume zao kitabia na hasa katika suala zima la utiifu. Bahati mbaya baadhi ya akina mama sio watiifu kwa waume zao na tena wengine wana dharau kubwa sana. Naam fahamu kwamba Mke si Mke bila Mume, na Mume si Mume bila Mke. Hata siku moja ndoa yako haiwezi kujengwa kwa kiburi au dharau kwa mumeo bali utakuwa unaumba jambo baya sana ndani ya mume wako.
Najua unaweza ukasema tabia za mume wangu ndiyo zinazifanya kumdharau, kumsema vibaya nk. Suala sio tabia zake, bali ni wewe kutumia hekima katika kukabiliana na tabia zisifofaa za mumeo kwa kuwa kumdharau ni kuendelea kubomoa na si kujenga, naam  ni kuendelea kuleta tatizo na sio kutatua tatizo. Umeshawahi kuwaza juu ya jambo hili kwamba, Mke anaagizwa kumtii mume wake kama vile kumtii Bwana. Imeandikwa katika Waefeso 5:22 ‘Enyi wake, watiini waume zenu kama kumtii Bwana wetu’. Je ni kweli ndivyo unavyomtii Mumeo? Naam haijalishi mume wako yukoje usionyeshe dharau, mtiii tu, ni mume wako.
Mtume Petro anawaonya wanawake akisema ‘kadhalika ninyi wake, watiini waume zenu; kusudi, ikiwa wako wasioliamini Neno, wavutwe kwa mwenendo wa wake zao, pasipo lile Neno’ (1Petro 3:1). Sijui kama wewe Msomaji unaona uzito uliopo kwenye mistari hii. Kwa lugha nyepesi utiifu wa mke kwa Mume utawafanya wengine kumwamini Yesu mnayemtumaini. Naam na upande wa pili, kukosa utiifu kwa mumeo kutawazuia wengine kumwamini Yesu, je unajua gharama ya kuwazuia wengine kumjua Kristo kwa sababu ya kukosa utiifu kwa mumeo (asomaye na afahamu siri hizi).
Wanaume kadhaa walioko kwenye ndoa wamekuwa wakiniambia kwenye suala la tabia hawajaona tofauti kati ya wanawake wasiokoka na waliokoka. Na kikubwa wanachosema ni kudharauliwa na wake zao. Hata kama katika hali ya kawaida mumeo anafanya mambo yanayopelekea wengine kumdharau wewe usifanye hivyo yeye ni kichwa chako
Fahamu kwamba daharau ni sumu mbaya kwenye ndoa yako yako mama, jizuie kabisa. Naam utiifu ni kila kitu kwa Mwanume, binafsi nimegundua wanachotafuta wanaume kwa wake zao bila kujali elimu zao, uchumi wao nk ni utiifu, naam kumdharau mumeo ni kubomoa nyumba yako ni kumruhusu Shetani kuharibu ndoa yako, ni kumuingiza mume wako fikra za wanawake wengine tofauti na wewe.
  • Kutunza siri za mume wako
Katika kuijenga nyumba yako ni lazima ujifunze kutunza, kuhifadhi na kuficha mapungufu ya mumeo kwa wengine. Naam hiyo ndiyo hekima. Baadhi ya akina mama   bila hata kujali wanaongea na nani, wamekuwa wakieleza mambo ya ndoa yao na siri za waume bila hata kujua athari yake. Naam kufanya hivyoni kubomoa na si kujenga. Unawajibika kmtii na kumtunzia mumeo siri zake licha ya mapungufu aliyo nayo na uzidi kumwomba Mungu kwamba aiponye ndoa yako.
2
Naam na hata kama ni muhimu uwaeleze kwa lengo la kujenga basi ni muhimu kuwe na mipaka ya nani unazungumza naye na nini unawaweleza maana si kila kitu wanapaswa kujua cha wewe na mumeo. Katika kulisistiza jambo hili Paulo anawagiza Tito akimweleza kwamba awatumie Wazee wa kike wenye mwenendo wa utakatifu ‘Ili wawatie wanawake vijana akili, wawapende waume zao, na kuwapenda watoto wao, na kuwa wenye kiasi, kuwa safi, kufanya kazi nyumbani mwao, kuwa wema, kuwatii waume zao wenyewe; ili neno la Mungu lisitukanwe’ (Tito 2:3-4).
  •  Matumizi ya kinywa chako
Mara kadhaa nimewasikia wanawake walioolewa wakisema maneno yasiyofaa kwa waume zao. Najua wengine ni kutokana na hasira na wengine kutokana na mfululizo wa matukio yasiyofaa ya mumewe. Nimesikiia wanawake wakiwaaita waume zao wajinga, wapumbavu, na mengine ambayo nisinependa kuandika hapa. Ninachotaka ukijue ni hiki, imeandikwa Mtu atashiba kwa matunda ya kinywa chake.
Tambua kwamba mume wako naye ana nafasi zake kama mwanandoa kwako, na nafasi moja wapo ni kuwa kichwa cha mwanamke. Sasa kila baya unalotamka kwake maana yake unaliumba kwenye kichwa chako mwenyewe na hivyo tarajia mabaya na uharibifu kwenye ndoa yako. Najua utaniambia Patrick kuna mambo yanaudhi sana na hayavumiliki, na mimi nitakujibu ni kweli lakini namna ya kushughulika nayo ni wewe kutumia hekima kama mjenzi na kuiponya ndoa yako na si kumesema vibaya.
Fahamu pia kwamba katika ulimwengu wa roho kuna pepo ambao kazi yao ni kufuatilia maneno/mawazo mabaya ambayo mtu anayanena ili kuyaumba yatimie. Mfano ukiwa na wazo kwamba kwamba Mume wangu si mzuri uwe una uhakika kuna pepo watakuja juu yako na kuhakikisha siku zote wana kufanya umuone mume wako mbaya.
Je hujasoma Zaburi 36: 4 inasemaje ‘Huwaza maovu kitandani pake, hujiweka katika njia mbaya; ubaya hauchukii”. Naam tafsiri yake ni kwamba hali ya sasa ya mtu huyo ni matokeo ya mawazo yake, naam mwanandoa huyu amewaza na kunena mabaya juu ya mume wake, na kwa sababu hiyo ameiingiza ndoa yake kwenye mabaya. Naam ni lazima ujifunze kunena mananeo yenye kuijenga ndoa yako na si kubomoa, ndivyo na nafsi yako, fikra zako zitakapokiri hivyo, naam ndivyo na BWANA Mungu naye atahakikisha hayo yanakujia.
  •  Msamaha (kusameheana)
Ndoa nyingi leo zinashida kwa sababu ya wanandoa kushindwa kusameheana.  Ni kweli kwenye ndoa kuna mambo mengi ambayo katika hali ya kibinadamu yanaweza kukufanya ushindwe kusamehe, nami kama Mwalimu sina budi kukufundisha kile ambacho neno la Mungu limeelekeza. Kumbuka imeandikwa tafuteni kwa bidii kuwa na amani na watu wote… (Waebrania 12:14). Naam watu wote wa kwanza akiwa na mumeo, hatutegemei uwe na mahusainao mazuri na watu wa nje, wakati mume wako hutaki kumsamehe, utakuwa unajidanganya nafsi yako.
8
Hivyo bila kujali Mumeo amefanya kosa ganii hakuna namna ni lazima ujifunze kusamehe na kusahau. Hii ni kwa sababu kutokusamehe ni kumpa Ibilisi nafasi ya kuendelea kuwavuruga. Si hivyo bali usitegemee kwamba hata maombi yenu nyote wawili yatakuwa yanasikilizwa. Maana kwa kushindwa kwako kusamehe una haribu mahusiano na Mungu (Mathayo 6:14) na kwa mwanaume kwa kushindwa kwake kukaa kwa akili na wewe kama mke, maandiko yanasema maombi yake hayatasikilizwa. Je unategemea nini kitatokea kama hautakuwa tayari kumsamehe.
  •  Kujali mahitaji ya mwenzako (tendo la ndoa)
Paulo Mtume aliwaandikia hivi wanandoa wa Korinto ‘Lakini kwa sababu ya zinaa kila mwanaume na awe na mke wake mwenyewe, na kila mwanamke na awe na mume wake mwenyewe. Mume na ampe mkewe haki yake, na vivyo hivyo mke na ampe mumewe haki yake. Mke hana amri juu ya mwili wake, bali mumewe; vivyo hivyo mume hana amri juu ya mwili wake, bali mkewe. Msinyimane isipokuwa mmepatana kwa muda, ili mpate faragha kwa kusali; mkajiane tena, Shetani asije akawajaribu kwa kutokuwa na kiasi kwenu’ (1Wakorinto 7:1-5).
Kimsingi andiko hili linalenga wanandoa wote wawili, bali kwa kuwa ujumbe huu ni maalum kwa wanawake nitaandika zaidi upande wa mwanamke. Biblia iko wazi kwamba kwa sababu ya zinaa (tendo la ndoa) kila mume awe na mke wake mwenyewe. Moja ya sababu muhimu za wewe kuolewa ni ili kumtosheleza mumeo kwa habari ya tendo la ndoa kama ilivyo na kwako pia.   
Kwa wanandoa wengi haja ya tendo la ndoa inatofautina, hata hivyo mara nyingi uhitaji wa tendo la ndoa kwa Mwanaume uko juu kuliko ilivyo kwa mwanamke. Hata hivyo kila mmoja ana – muhitaji mwenzake ili kutoshelezwa katika hitaji hili muhimu. Baadhi ya wanawake kwa kujua ukweli huu na tofauti hii ya uhitaji wa tendo la ndoa, kwa kutokufikiri athari zake kwa wenzi wao, kwao binafsi na ‘future’ yao huwanyima waume zao haki yao ya tendo la ndoa hasa pale wanapokuwa wametofautiana juu ya jambo fulani. Mbaya zaidi wapo akina mama ambao wakikasirika huwanyima waume zao haki hii ya msingi kwa muda mrefu kwa mfano mwezi mmoja, minne, hata zaidi ya mwaka na wanaishi nyumba moja na wengine wanalala kitanda kimoja.   
Mume wako akijua kwamba unatumia ugomvi/tofauti zenu au hata kwa makusudi kumnyima haki yake ya tendo la ndoa, na jambo hilo likawa endelevu uwe na uhakika taratibu unaanza kuharibu ndoa yako. Maana, Shetani ni mzuri sana wa kutumia nafasi ambazo wana wa Mungu wanampa. Ndani ya mume wako yataingia mawazo mabaya (Ezekieli 38:10) na kumweleza ‘je mbona kuna wanawake wengi, ni suala la kwenda kumaliza haja yako kwa mwanamke yoyote mwingine’. Wazo jingine pia litamwambia kwa nini huyu mwanamke akutese kiasi hiki, kwa nini usiwe na nyumba ndogo nk. Uwe na uhakika endapo mumeo ameokoka, hofu ya Mungu ndani yake ndiyo itakayomzuia kufanya mambo haya lakini ukimuuliza taratibu atakuambia mawazo haya hunijia mara kwa mara unaponinyima haki yangu ya tendo la ndoa.
6
Naam, hata kama hatafanya hayo, uwe na uhakika kwamba tayari kwenye ufahamu wake umeshapanda mbegu mbaya na itaendelea kukua endapo utaendelea na tabia yako ya kumnyima haki yake. Ndiyo, usishangae siku moja kukuta mumeo ametoka nje ya ndoa, usikimbilie kumlaumu Shetani, maana wewe ndiye ulifungua mlango na kumkaribisha. Nakumbuka mwanandoa mmoja (Mwanaume) alisema hizi ndoa za Kikristo zinatutesa sana wanaume, na zinawafanya hawa wanawake wajisahau sana, kwa kuwa wanajua Biblia imetuzia kuoa mke zaidi ya mmoja. Naam ilibidi nitumie muda mwingi kurejesha ufahamu wa huyu ndugu kwenye msingi wa ki-Mungu kwa kuwa nilijua tayari kuna wazo lilishaingia moyoni mwake na nilijua wapi linampeleka.
Nimeandika jambo hili kwa kirefu kwa sababu mara nyingi sehemu kubwa ya kesi za wanandoa inapofika kwenye suala la unyumba, wanawake ndio wanao – wanyima waume zao. Naam nakiri hata wanaume wapo lakini ni mara chache sio kama ilivyo kwa wanawake. Mwanamke sikia, kitendo cha Mungu kukupa huyo mume ni heshima ya pekee sana kwamba ni wa kwako pekee yako. Ukitaka kujua gharama yake waulize wanawake ambao wana ‘share’ mume namna inavyowagharimu kihisia, kifikra na kimaisha. Naam ni lazima ujifunze kujali na kutimiza mahitaji ya mwenzi wako vinginevyo unafungua mlango kwenye ufahamu wa mumeo na kumwambia angalia kule nje kuna wanawake wengine (Asomaye na afahamu).
Ukweli ni kwamba kuna sababu mbalimbali ambazo hupelekea wanawake kwenye ndoa kufanya hivyo, ila ushauri wangu ni kwamba, uamuzi wa namna hii (kumnyima tendo la ndoa mumeo) ni wa kuharibu na si kujenga. Hivyo haijalishi huyo baba kakukosea nini (labda ziwe issue za kiafya), suala la tendo la ndoa kwake ni muhimu sana na ni haki yake, kutokumpa haki yake ni kukaribisha Shetani kwenye ndoa yako. Naam ni vizuri mka-hakikisha kwamba tofauti zenu zote mna – zimaliza kabla hamjaingia kulala, itawasaidia sana.
Kuna maeneo ambayo ningeweza kuandika pia, lakini hayo matano hapo juu ni msingi wa mengine mengi. Kutokana na urefu wa nafasi hii ya Mwanamke kama Mjenzi nimelazimika kuigawanya mara mbili kwa hiyo katika sehemu ya tano nitamalizia kipande kilichobaki ambacho ndani yake nitaonyesha mwanamke anawezaje kupata hekima ya kumsaidia kuafanya haya na nitaweka baadhi ya mifano yenye kusaidia.

No comments:

UHURUTZ. Theme images by hanoded. Powered by Blogger.