Ads Top

Dar es Salaam/Arusha. Utata wa kidiplomasia ulioibuka kuhusu raia wa kigeni kukamatwa wakituhumiwa kwa mlipuko wa bomu katika Kanisa Katoliki umemlazimu Waziri wa Mambo ya Nchi za Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe kutua jijini Arusha kusawazisha mambo

Membe alisema jana kuwa atakwenda huko kufuatilia suala hilo na hasa kwa kukamatwa raia wa kigeni wakihusishwa na tukio hilo, wakiwa ni miongoni mwa watu 12 wanaoshikiliwa na polisi wakituhumiwa kuhusika na shambulio hilo lililoua watu watatu na wengine zaidi ya 60 kujeruhiwa.
“Ninakwenda Arusha kesho (leo) ili kufahamu undani wa suala hili. Baada ya kwenda ndiyo nitakuwa katika nafasi ya kuongelea mambo haya,” alisema Membe wakati alipoulizwa jana kuhusu malalamiko ya nchi za Saudi Arabia na Falme za Kiarabu (UAE) kuhusu kukamatwa kwa raia wao.
Watu wanaoshikiliwa na polisi kwa tuhuma hizi ni pamoja nja Victor Ambrose Calist (20), Mwendasha Bodaboda na mkazi wa Kwa Mrombo, Jeseph Yusuph Lomayani (18) mwendesha Bodaboda, Mkazi wa Kwa Mrombo jijini  Arusha.
Wegine ni George Batholomeo Silayo (23), mfanyabiashara na mkazi wa Olasiti, Arusha, Mohamed Sulemani Said (38) mkazi wa Ilala, Dar es Salaam na Jassini Mbaraka (29) mkazi wa Arusha.
Wale wanaotuhumiwa kutoka nje ya Tanzania ni pamoja na raia wa Falme za Kiarabu (UAE), Said Abdalla Said (28), Abdulaziz Mubarak (30) na Said Mohsen wakati Jassini Mbaraka (29) anatokea Saudi Arabia
Hata hivyo, suala la kukamatwa kwa raia wa nchi za kigeni limezua utata wa kidiplomasia kutoka nchi za Saudi Arabia na UAE.
Gazeti dada la The East African limekariri vyanzo vyake vikidai kuwa mabalozi wa nchi hizo wanataka kuandika barua ya malalamiko kwa Serikali ya Tanzania kupinga kukamatwa kwa raia wao, pia kutangazwa kwenye vyombo vya habari.
Mabalozi wa nchi hizo za Mashariki ya Kati walifuatana na wanasheria wao kwenda kuangalia hali za watuhumiwa kutoka nchi zao huko Arusha.
Balozi wa Saudi Arabia, Hani Abdalla Momenah aliliambia gazeti la Al-Hayat la Saudi Arabia akidai mtu wake alikamatwa kwa hisia tu na kwamba asingeondoka Arusha hadi kieleweke.
“Watu hawa wamekamatwa kwa hisia tu ila nina uhakika wataachiwa kwa mapenzi ya Mungu. Walikuwa wamekuja kutalii Tanzania,” aliongeza Momenah.
Wakati mtuhumiwa raia wa Tanzania Ambrose anayetuhumiwa kwa kumbeba kwenye pikipiki ndiye aliyehusika na ulipuaji.
Hatima kujulikana leo
Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Arusha, Liberatus Sabas aliliambia Mwananchi jana kuwa taarifa kamili za watuhumiwa wa tukio hilo zitatolewa leo kama waliokamatwa watafikishwa mahakamani au la.
“Kesho (leo) tutatoa taarifa zote, uchunguzi ulipofikia na watuhumiwa wote baada ya upelelezi,” alisema Kamanda Sabas.
Wasiwasi makanisani
Ikiwa ni wiki moja baadaa ya mlipuko huo, hofu ilitanda katika makanisa mbalimbali jijini Arusha huku ulinzi ukiimarishwa wakati wa ibada jana. Baadhi ya askari walitoka Chuo cha Polisi Moshi kuongeza ulinzi.

No comments:

UHURUTZ. Theme images by hanoded. Powered by Blogger.