Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), kimesema kitaanzisha kambi nchi nzima kwa ajili ya kuwapa mafunzo maalumu walinzi wa chama hicho ‘Red Brigade’, ili waweze kuwalinda viongozi na wanachama wake
Kimesema kimechukua hatua hiyo kwa madai kwamba Serikali na vyombo vyake vya ulinzi na usalama vimeshindwa kufanyia kazi malalamiko yake kuhusu mauaji, vitisho na matukio ya kutisha wanayofanyiwa baadhi ya viongozi na wanachama wake.
“Ni wajibu wa chama kutafuta njia za kujilinda,
hatulindwi na Jeshi la Polisi, Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) wala
Usalama wa Taifa, watu wetu wanapigwa na wanauawa hata tukienda polisi
hatupati haki yetu. Ni bora tuanzishe mafunzo na tujilinde wenyewe kwani
tukiendelea kupiga magoti na kulia tutakuwa wajinga,” alisema
Mwenyekiti wa chama hicho, Freeman Mbowe.
Aidha, chama hicho kimewataka wabunge wake wote
kushirikiana na wabunge wengine wenye mapenzi mema na nchi, kupitia
Bunge la Jamhuri ya Muungano kuanzishe mchakato wa kupiga kura ya
kutokuwa na imani na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda.
Uamuzi huo unatokana na kauli ya Waziri Mkuu Pinda
aliyoitoa Juni 19, mwaka huu katika Kipindi cha Maswali ya Papo kwa
Hapo kwa Waziri Mkuu Bungeni Mjini Dodoma alipoviagiza vyombo vya dola
kuwashughulikia kwa kuwapiga wale watakaokataa kutii amri wakati
wakifanya vitendo vya uvunjifu wa amani.
Akisoma maazimio ya Kikao cha Kamati Kuu (CC) ya
chama hicho kilichofanyika Dar es Salaam Julai 6 na 7, Mbowe alisema
wanaanzisha mafunzo hayo ili kukabiliana na fujo zinazofanywa na walinzi
wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) ‘Green Guards’ ambao alidai katika kambi
zao wamepewa mafunzo ya kushambulia raia, hasa wanachama wa Chadema.
“Ili kukabiliana na fujo zinazofanywa na vijana wa
CCM ‘Green Guards’, sisi tuna kikosi cha ‘Red Brigade’ ambacho ni
kikosi kilichoundwa kwa mujibu wa katiba ya chama kwa ajili ya kulinda
mali za chama, labda kimekuwa legelege au kimezidi upole ndiyo maana
tunapigwa sana,” Mbowe alisema na kuongeza:
“Tutafanya mafunzo maalumu ya vijana wetu nchi
nzima, tutawafundisha namna ya kujilinda, tutaweka kambi kama CCM
wanavyoweka kambi kufundisha vijana wao namna ya kushambulia. Hatuwezi
kuendelea kuwa mbuzi wa kafara.”
Viongozi wa CCM hawakupatikana jana kuzungumzia
kambi hizo zilizotajwa na Chadema kwani simu za Naibu Katibu Mkuu
(Bara), Mwigulu Nchemba na Katibu wa Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye
ziliita bila ya kupokewa.
Alisema kambi ya chama hicho itakuwa maalumu kwa ajili ya kuwafundisha vijana ukakamavu na jinsi ya kujilinda.
Msajili wa Vyama vya Siasa, John Tendwa
hakupatikana jana kuzungumzia hatua hiyo ya Chadema kwani simu yake ya
mkononi ilikuwa haipatikani.
Katika maelezo yake, Mbowe alisema viongozi wa
chama hicho wamekuwa wakionewa katika matukio mbalimbali na kudai kwamba
hata wanapokwenda polisi kutoa taarifa hukamatwa na kushtakiwa. Alisema
katika mwelekeo huo, zaidi ya makada 2000 wa chama hicho
wameshafunguliwa kesi katika Mahakama mbalimbali nchini.
Alitolea mfano wa tukio la mlipuko wa bomu wakati chama hicho
kikihitimisha kampeni zake za uchaguzi wa udiwani katika Viwanja vya
Soweto, Arusha Juni 15 mwaka huu, akisema licha ya yeye na Mbunge wa
Arusha Mjini, Godbless Lema kushambuliwa, mpaka leo hakuna aliyekamatwa
na wala Serikali haijaeleza nini kilichotokea.
Alisema mpaka sasa Rais Jakaya Kikwete amekaa kimya na hajaunda tume huru ya kimahakama kuchunguza kwa uwazi shambulio hilo.
Alisema hata Ofisi ya Bunge haikushiriki katika
tukio hilo la msiba huo wala kutoa mchango kwa wafiwa na walioathirika
kinyume na taratibu zilizowekwa na Bunge za kutambua na kushiriki katika
majanga na misiba ya aina hiyo.
Akizungumzia kauli ya Waziri Mkuu, Mbowe alilitaka
jeshi la polisi kupuuza kauli hiyo katika utekelezaji wa kazi zake,
huku akisema kauli hiyo ni uvunjifu wa amani.
Alisema kauli hiyo inatoa baraka wa polisi
kuendelea na vitendo vya ukatili na mauaji dhidi ya wananchi na
kulifanya kutangazwa kuwa moja ya majeshi katili ya polisi katika Afrika
Mashariki.
“Kauli yake inakiuka Katiba na sheria za nchi yetu
zinazokataza jeshi hilo kutumia nguvu dhidi ya raia wasiokuwa na silaha
ambao wanatumia haki zao za kikatiba kufanya maandamano,” alisema.
Polisi wanena
Akizungumzia kauli hiyo ya Chadema, Msemaji wa
Jeshi la Polisi nchini, Advera Senso alikitika chama hicho kiache
kuwapotosha Watanzania.
“Jeshi la Polisi lipo kwa mujibu wa sheria na
linalinda watu wote bila kujali chama chochote cha siasa na litaendelea
kubaki katika nafasi yake, hayo wanayoyasema ni hisia zao tu, ila amani
ipo na ndiyo maana hata wao wameweza kuwaita na kuzungumza na nyinyi
(wanahabari) kwa amani,” alisema.
No comments: