Ads Top

Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), kimesema kitaanzisha kambi nchi nzima kwa ajili ya kuwapa mafunzo maalumu walinzi wa chama hicho ‘Red Brigade’, ili waweze kuwalinda viongozi na wanachama wake


Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe akionyesha kitabu chenye mkusanyiko wa matukio ya wanachama wake kuumizwa na wengine kupoteza maisha kwa madai ya kupigwa na polisi, alipo zungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam jana. Picha na Michael Jamson  

Kimesema kimechukua hatua hiyo kwa madai kwamba Serikali na vyombo vyake vya ulinzi na usalama vimeshindwa kufanyia kazi malalamiko yake kuhusu mauaji, vitisho na matukio ya kutisha wanayofanyiwa baadhi ya viongozi na wanachama wake.
“Ni wajibu wa chama kutafuta njia za kujilinda, hatulindwi na Jeshi la Polisi, Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) wala Usalama wa Taifa, watu wetu wanapigwa na wanauawa hata tukienda polisi hatupati haki yetu. Ni bora tuanzishe mafunzo na tujilinde wenyewe kwani tukiendelea kupiga magoti na kulia tutakuwa wajinga,” alisema Mwenyekiti wa chama hicho, Freeman Mbowe.
Aidha, chama hicho kimewataka wabunge wake wote kushirikiana na wabunge wengine wenye mapenzi mema na nchi, kupitia Bunge la Jamhuri ya Muungano kuanzishe mchakato wa kupiga kura ya kutokuwa na imani na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda.
Uamuzi huo unatokana na kauli ya Waziri Mkuu Pinda aliyoitoa Juni 19, mwaka huu katika Kipindi cha Maswali ya Papo kwa Hapo kwa Waziri Mkuu Bungeni Mjini Dodoma alipoviagiza  vyombo vya dola kuwashughulikia kwa kuwapiga wale watakaokataa kutii amri wakati wakifanya vitendo vya uvunjifu wa amani.
Akisoma maazimio ya Kikao cha Kamati Kuu (CC) ya chama hicho kilichofanyika Dar  es Salaam Julai 6 na 7, Mbowe alisema wanaanzisha mafunzo hayo ili kukabiliana na fujo zinazofanywa na walinzi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) ‘Green Guards’ ambao alidai katika kambi zao wamepewa mafunzo ya kushambulia raia, hasa wanachama wa Chadema.
“Ili kukabiliana na fujo zinazofanywa na vijana wa CCM ‘Green Guards’, sisi tuna kikosi cha ‘Red Brigade’ ambacho ni kikosi kilichoundwa kwa mujibu wa katiba ya chama kwa ajili ya kulinda mali za chama, labda kimekuwa legelege au kimezidi upole ndiyo maana tunapigwa sana,” Mbowe alisema na kuongeza:
“Tutafanya mafunzo maalumu ya vijana wetu nchi nzima, tutawafundisha namna ya kujilinda, tutaweka kambi kama CCM wanavyoweka kambi kufundisha vijana wao namna ya kushambulia. Hatuwezi kuendelea kuwa mbuzi wa kafara.”
Viongozi wa CCM hawakupatikana jana kuzungumzia kambi hizo zilizotajwa na Chadema kwani simu za Naibu Katibu Mkuu (Bara), Mwigulu Nchemba na Katibu wa Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye ziliita bila ya kupokewa.
Alisema kambi ya chama hicho itakuwa maalumu kwa ajili ya kuwafundisha vijana ukakamavu na jinsi ya kujilinda.
Msajili wa Vyama vya Siasa, John Tendwa hakupatikana jana kuzungumzia hatua hiyo ya Chadema kwani simu yake ya mkononi ilikuwa haipatikani.
Katika maelezo yake, Mbowe alisema viongozi wa chama hicho wamekuwa wakionewa katika matukio mbalimbali na kudai kwamba hata wanapokwenda polisi kutoa taarifa hukamatwa na kushtakiwa. Alisema katika mwelekeo huo, zaidi ya makada 2000 wa chama hicho wameshafunguliwa kesi katika Mahakama mbalimbali nchini.
Alitolea mfano wa tukio la mlipuko wa bomu wakati chama hicho kikihitimisha kampeni zake za uchaguzi wa udiwani katika Viwanja vya Soweto, Arusha Juni 15 mwaka huu, akisema licha ya yeye na Mbunge wa Arusha Mjini, Godbless Lema kushambuliwa, mpaka leo hakuna aliyekamatwa na wala Serikali haijaeleza nini kilichotokea.
Alisema mpaka sasa Rais Jakaya Kikwete amekaa kimya na hajaunda tume huru ya kimahakama kuchunguza kwa uwazi shambulio hilo.
Alisema hata Ofisi ya Bunge haikushiriki katika tukio hilo la msiba huo wala kutoa mchango kwa wafiwa na walioathirika kinyume na taratibu zilizowekwa na Bunge za kutambua na kushiriki katika majanga na misiba ya aina hiyo.
Akizungumzia kauli ya Waziri Mkuu, Mbowe alilitaka jeshi la polisi kupuuza kauli hiyo katika utekelezaji wa kazi zake, huku akisema kauli hiyo ni uvunjifu wa amani.
Alisema kauli hiyo inatoa baraka wa polisi kuendelea na vitendo vya ukatili na mauaji dhidi ya wananchi na kulifanya kutangazwa kuwa moja ya majeshi katili ya polisi katika Afrika Mashariki.
“Kauli yake inakiuka Katiba na sheria za nchi yetu zinazokataza jeshi hilo kutumia nguvu dhidi ya raia wasiokuwa na silaha ambao wanatumia haki zao za kikatiba kufanya maandamano,” alisema.
Polisi wanena
Akizungumzia kauli hiyo ya Chadema, Msemaji wa Jeshi la Polisi nchini, Advera Senso alikitika chama hicho kiache kuwapotosha Watanzania.
“Jeshi la Polisi lipo kwa mujibu wa sheria na linalinda watu wote bila kujali chama chochote cha siasa na litaendelea kubaki katika nafasi yake, hayo wanayoyasema ni hisia zao tu, ila amani ipo na ndiyo maana hata wao wameweza kuwaita na kuzungumza na nyinyi (wanahabari) kwa amani,” alisema.

No comments:

UHURUTZ. Theme images by hanoded. Powered by Blogger.