Kaimu Afisa Habari Misungwi afukuza Waandishi wa Habari kikao cha Baraza la Madiwani
Na
Mwandishi wetu Mwanza.
KAIMU Afisa Habari wa Wilaya ya Misungwi Thomas Lutego
amewafukuza Waandishi wa Habari wa Gazeti la Tanzania Daima Antony Sollo na
Valence Robert pamoja na Twallad Sallum wa Gazeti la Mwananchi waliofika katika
ukumbi wa Shule ya Sekondari ya Misungwi ambako kikao cha Baraza la Madiwani
kilikuwa kikifanyika hapo.
Waandishi hao waliwasili katika ukumbi huo na kukuta kikao
cha Baraza la Madiwani kikiendelea na kuingia kwa ajili ya kutekeleza majukumu
yao ya kupasha habari kwa jamii, ghafla Lutego aliwaita waandishi hao na
kuwaeleza kuwa hawaruhusiwi kushiriki kikao hicho kwa kuwa alikuwa amealika
waandishi wa habari vyombo vine.
“Naomba mtoke ninyi mmealikwa na nani? mimi nilikuwa
nimealika waandishi wane tu sasa nawaonya iwapo mtaendelea kukaa na kufanya
shughuli zenu hapa mtaona nitakachowafanya.”alisema Lutego.
Baada ya kutokea kwa mtafaruku huo Waandishi walitoa ripoti
kwa Mkuu wa Wilaya ya Misungwi Mariam Lugayila ili aweze kuwapa
mwongozo, Lugayila alisema “kikao hiki ni kikao cha wazi sasa kwa nini awazuie?
Jamani mimi msije mkaninukuu ila ninavyofahamu mimi kikao hiki ruksa mtu yeyote
kuhudhuria na kufuatilia mambo mbalimbali.” inakuwaje sasa mtu achukue jukumu la
kufukuza wanahabari?
Hali hii si mara ya kwanza kwa Afisa Habari huyu kufanya
fitna kwa waandishi wa Habari na inaonekana kuna kitu kinachofichwa na Afisa
Habari huyo ili watu wasijue kinachoendelea katika Halmashauri hiyo.
Imedaiwa kuwa halmashauri ya Wilaya ya Misungwi imekuwa na
matukio mengi ya ufujaji wa fedha za umma na huenda kualika waandishi kwa
ubaguzi ni moja ya njia ya kuzuia na kuficha maovu hayo na wameomba Mkurugenzi
wa Halmashauri achukue hatua kutatua mgogoro huo kama na yeye hahusiki kwa
namna moja au nyingine katika suala la kuzuia waandishi.
Akizungumza na Tanzania daima Diwani wa Kata ya Usagara
Costantine Kilaga alisema “huyu bwana atakuwa na maslahi binafsi juu ya jambo
hili hiki ni kikao huru na ni cha wazi sasa kwa nini azuie waandishi? alihoji
Kilaga”
Katika kikao cha baraza la Madiwani wa Halmashauri hiyo
kilichopita Lutego alitoa taarifa za kutumia kiasi cha shilingi laki sita
600,000 tu kati ya shilingi milioni nane 8,000,000. zinazotengwa na Halmashauri kwa ajili ya masuala ya Habari kwa mwaka 2013.
Hali hii inaonyesha jinsi anavyowanyima haki ya kupata
habari wananchi wa Wilaya ya Misungwi na pia ni ushahidi tosha kwamba kuna siri
kubwa inayofichwa na huenda siyo maamuzi yake ila kuna kitu nyuma yake.
Wakiendelea kutafuta haki yao ya kuhudhuria kikao
hicho, waandishi wa Habari hao walimpa taarifa Mbunge wa Jimbo la Misungwi
Charles Kitwanga juu ya kunyimwa haki hiyo ambapo Kitwanga alimwita Afisa
habari huyo na kumhoji na baada ya muda Lutego alionekana kulegeza msimamo wake
huo na kuwaacha waandishi hao kuendelea na majukumu yao.
Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Misungwi Nathan
Mshana alipoulizwa iwapo kuna uhalali juu ya kauli iliyotolewa na Kaimu Afisa
Habari Thomas Lutego kuzuia waandishi kuingia katika kikao cha Madiwani hao
Mshana alisema hana cha kuzungumza juu ya jambo hili alijibu kwa mkato “Kikao
hiki ni cha wazi na kwamba kila mtu anayo haki ya kuingia katika kikao
hicho.” alisema Mshana.
Chanzo cha taarifa hizi kinaendelea kufuatilia kujua
undani wa chanzo cha ubaguzi kwa wanahabari unaofanywa na Afisa Habari huyo kwa
kuita waandishi kirafiki huku akiacha kuwaalika wanahabari wengine kuhudhuria
vikao mbalimbali vya Halmashauri hiyo.
No comments: