Ads Top

Shirika la Viwango nchini (TBS), limekifungia kiwanda cha kutengeneza chumvi cha Sea Salt


Shirika la Viwango nchini (TBS), limekifungia kiwanda cha kutengeneza chumvi cha Sea Salt kilichopo karibu na Hifadhi ya Saadan Wilaya ya Bagamoyo mkoani Pwani.

TBS imechukua hatua hiyo baada ya kubainika kuwa chumvi hiyo ina ukosefu mkubwa wa madini joto.

Ukosefu wa madini joto kwenye chumvi husababisha watumiaji wake kuugua ugonjwa wa tezi ya shingo.

Akizungunza na waandishi wa habari jana, Ofisa Mdhibiti Ubora TBS, Deusdedith Paschal, alisema kiwanda hicho kitaruhusiwa kuendelea na uzalishaji baada ya kurekebisha kasoro hiyo kwa kuongeza madini joto ndani ya chumvi hiyo.

"Serikali imekuwa ikisisitiza wananchi kutumia madini joto na chumvi hii ina upungufu mkubwa wa madini joto na ndiyo maana tumeamua kuchukua hatua kwa kukifungia kiwanda," alisisitiza.

Aidha, alisema baada ya kupimwa chumvi hiyo katika maabara yao, wamebaini kuwapo kwa mchanga mwingi kwenye bidhaa hiyo, jambo ambalo halitakiwi.

"Chumvi inapotumiwa, inatakiwa iyeyuke, lakini hii haiyeyuki yote, kuna mchanga unaonekana na hii inasababishwa na mazingira ya kiwanda hayapo vizuri," alifafanua Paschal.


Alisema hatua inayofuata sasa, ni kukusanya chumvi yote iliyosambawa sokoni ili wananchi wasiinunue na kuitumia.

Kwa upande wake, Mkuu wa Kitengo cha Habari TBS, Roida Andusamile, alisema kiwanda hicho kimekiuka utaratibu na kwamba kitachukuliwa hatua kali kwa mujibu wa Sheria za TBS.

Andusamile alisema ukaguzi huo ni mwendelezo kwa viwanda vingine.

Hata hivyo, Mhasibu wa kiwanda hicho, Daud Chaula, alisema chumvi inayozalishwa hapo, ina madini joto na kwamba wameshindwa kuielewa TBS kuchukua hatua ya kukifunga.

Kwa mujibu wa Chaula, kiwanda hicho kina uwezo wa kuzalisha tani 2,500 za chumvi kwa mwezi ambapo kati ya kiasi hicho, tani 2,000 husafirishwa kwenda nje ya nchi na kiasi kinachobaki huuzwa hapa nchini.

"Kiwanda chetu huzalisha chumvi kwa kuzingatia taratibu zote na soko letu kubwa liko nje ya nchi...Hatuwaelewi TBS kwanini wamechukua hatua ya kikifunga," alisema Chaula.
SOURCE: NIPASHE

No comments:

UHURUTZ. Theme images by hanoded. Powered by Blogger.