POLISI WAWATAWANYA WAFANYAKAZI WA KAMPUNI YA CHICCO WALIOANDAMANA WAKIDAI HAKI YAO KAGERA.
Jeshi la Polisi mkoani Kagera limelazimika kutumia nguvu katika
kuwatawanya baadhi ya wafanyakazi wa kampuni ya ujenzi ya CHICCO toka
nchini China inayojenga barabara ya kiwango cha lami yenye urefu wa
kilomita hamsini na tisa toka Kyaka hadi Bugene ambao ni miongoni mwa
wafanyakazi zaidi ya mia tano wanaoidai kampuni hiyo zaidi ya shilingi
bilioni moja.
Mkuu wa jeshi la polisi wa wilaya ya Karagwe Miki Makanja akitoa
onyo kabla ya jeshi hilo kuwatawanya wafanyakazi hao kwa mabomu na maji
ya kuwasha waliokuwa wakifanya maandamano kuelekea kwenye ofisi za
kampuni hiyo kudai haki yao aliwaambia warudi majumbani mwao au warudi
kwenye maeneo ya kazi kwa kuwa madai yao yanashughulikiwa na ofisi ya
mkuu wa wilaya hiyo kauli iliyopigwa vikali.
Nao baadhi ya wafanyakazi walioongea na ITV wakati wakielezea
sababu za kufanya maandamamo wameyataja madai yao ya tangu mwaka 2013
ambayo hayajalipwa na kampuni ya ukandarasi ya CHICCO kuwa ni pamoja na
mapunjo ya mishahara, fedha za kuachishwa kazi, fedha za muda wa kazi ya
ziada na fedha za likizo, pia wamelalamikia vitendo ambavyo hufanyiwa
vya unyayasaji pale wanapodai haki yao ambavyo wamevitaja kuwa ni
kuachishwa kazi bila sababu.
Kufuatia vurugu hizo meneja wa kampuni ya CHICCO aliamua kujificha
na hakutaka kuongea na ITV iliyokuwa kwenye eneo la tukio, hata hivyo
ITV ilifanikiwa kumpata mwakilishi wa kampuni ya TECU inayosimamia mradi
wa ujenzi wa barabara hiyo, mhandisi Mashubila Kamuhabwa, akizungumza
amesema ya madai ya wafanyakazi hao kuwa ni halali na yanashughulikiwa,
amesema kampuni hiyo iko kwenye mchakato wa kulipa madai ya wafanyakazi
hao wakati wowote kuanzia sasa.
chanzo ITV
No comments: