WAFANYABIASHARA WANAOKWEPA KULIPA KODI NCHINI, WAJIANDAE KUFUNGIWA BIASHARA
Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha, Dk. Servacius Likwelile.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha, Dk. Servacius Likwelile (pichani),
amesema wafanyabiashara wanaokwepa kulipa kodi nchini, wajiandae
kufungiwa biashara zao kutokana na kurudisha nyuma maendeleo ya nchi.
Akizungumza na baadhi ya wafanyabiashara na maafisa wa Mamlaka ya
Mapato (TRA) jijini Mwanza mwishoni mwa wiki, Dk. Likwalile alisema
wafanyabiashara wengi wamekuwa wakifanya biashara na kukwepa kulipa kodi
ambayo inasaidia maendeleo ya nchi.
“Hivi sasa kila sehemu tumeweka watu wetu ili kuwafuatilia wale
wasiolipa kodi…hivyo mfanyabiashara asiyelipa kodi ajiandae kufungiwa
biashara yake,” alisema Dk. Likwelile.
Aidha, Dk. Likwalile aliwataka wafanyabiashara kushirikiana na
maafisa wa TRA katika kukusanya mapato ili kuiletea maendeleo nchi.
Alisema sifa ya mfanyabiashara mzuri ni kuhakikisha analipa kodi
badala ya kukwepa, pia kuonyesha uzalendo ili kuiletea nchi maendeleo
kwa kasi.
“Tuwe na uchungu na nchi yetu, tuhakikisha kila mtu analipa
kodi…zipo hoteli kubwa na nzuri, lakini hazitoi malipo ya stakabadhi
hivyo kuibia nchi mapato,” alisema.
Hata hivyo, aliwataka wafanyabiashara kuhakikisha wanatoa
stakabadhi pale wanapofanya biashara zao na wala wasidhani kutoa
stakabadhi hizo ni kufanya hisani kwa mteja.
Dk. Likwelile alisema mapato yanayokusanywa na TRA yanasaidia
kulipa mishahara kwa wafanyakazi wa serikali zaidi ya Sh. bilioni 535
kwa mwezi mmoja.
Naye mfanyabiashara Abubakar Hassan, aliishauri TRA kuachana na
vitisho wakati wa ukusanyaji wa kodi ambayo ni haki ya kila
mfanyabiashara kufanya hivyo.
No comments: