Ads Top

WAZIRI MKUU, KASSIM MAJALIWA, ANATARAJIWA KUFUNGUA MKUTANO WA WADAU WA UWEZESHAJI WANANCHI KIUCHUMI

 
waziri mkuu Kasimu Majaliwa
 
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa, anatarajiwa kufungua mkutano wa wadau wa uwezeshaji wananchi kiuchumi jijini Dar es Salaam leo.
Akizungumza na waandishi wa habari,  Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu, Dk. Hamisi Mwinyimvua, alisema mkutano huo ni sehemu ya utaratibu na utekelezaji wa Sera ya Taifa ya Uwezeshaji.
Alisema mkutano huo unaotayarishwa na Baraza la Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi (NEEC) na Ofisi ya Waziri Mkuu utahusisha wadau mbalimbali ambao ni wizara, idara na taasisi za serikali, mamlaka za serikali za mitaa, mashirika yasiyo ya kiserikali na sekta binafsi.
Kwa mujibu wa Dk. Mwinyimvua, pamoja na mambo mengine, mkutano huo utajadili taarifa ya utekelezaji wa sera ya taifa ya uwezeshaji wananchi kiuchumi na kutambua juhudi za wadau wanaotekeleza sera hiyo.
“Mkutano pia utajadili changamoto na kuibua mbinu bora za utekelezaji wa mkakati wa taifa wa uwezeshaji wananchi kiuchumi,” alisema na kuongeza kuwa mikutano kama hiyo itakuwa inafanyika kila mwaka.
Naye Katibu Mtendaji wa NEEC, Beng’i Issa, alisema kupitia mkutano huo, baraza hilo linatarajia kuanzisha rasmi dawati la uwezeshaji na ushiriki wa wananchi kuanzia ngazi ya wilaya, mkoa, wizara na idara katika kufuatilia masuala ya uwezeshaji, kuandaa taarifa na  kuwasilisha NEEC.
“Mkutano huu utasaidia kuratibu majukumu ya uwezeshaji kwa kuzingatia uwajibikaji, uadilifu, uaminifu na kujali,” alisema.
Beng’I aliongeza kusema kuwa, mkutano huo pia utachochea hamasa na kuhakikisha wananchi wanapewa upendeleo wa kipekee kwa watoa huduma mbalimbali katika zabuni na miradi mikubwa katika maeneo yao pale wanapokidhi masharti ya zabuni husika.
Baraza hilo limesandaa mkakati wa taifa wa uwezeshaji wananchi kiuchumi na mwongozo wake unaohusisha sekta zote nchini utazinduliwa katika mkutano huo.
chanzo nipashe

No comments:

UHURUTZ. Theme images by hanoded. Powered by Blogger.