RAIS MAGUFULI NA RAIS MUSEVENI WAMEKUBALIANA IKULU NDOGO LEO ARUSHA
President wa jamhuri ya muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli ambaye pia ni mwenyekiti wa Jumuiya ya Afrika Mashariki amekutana na kufanya Mazungumzo na Rais wa Uganda Yoweri Museveni ambapo pamoja na mambo mengine wamekubaliana kujengwa kwa bomba la kusafirisha mafuta kutoka Bandari ya Tanga Tanzania hadi nchini Uganda.
Rais Museveni amemtembelea Rais Magufuli
katika Ikulu ndogo ya Arusha leo jioni mara baada ya kuwasili hapa
nchini akitokea nchini Uganda, ambapo hapo kesho atahudhuria mkutano
mkuu wa 17 wa kawaida wa wakuu wa nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika
Mashariki.
Baada ya wawili hawa kufanya mazungumzo ya faragha, Rais Magufuli amesema wamekubaliana kutekeleza mradi huo wa bomba la kusafirisha mafuta kutoka Tanga hadi Uganda kwa manufaa ya nchi zote mbili na nchi nyingine za Afrika Mashariki, litakuwa na urefu wa kilometa 1,120 na kwamba mradi huo utazalisha ajira za watu zaidi ya 15,000.
Rais Magufuli ameongeza kuwa pamoja na kujengwa kwa
bomba la mafuta, pia wamezungumzia kuongeza biashara ndani ya nchi za
jumuiya ya Afrika Mashariki, kujenga viwanda na kuzalisha ajira zaidi
kupitia sekta mbalimbali za uzalishaji mali.
Rais Magufuli amesema katika mkutano huu nchi wanachama watajadili maombi ya nchi ya Sudan Kusini
kupata uanachama ndani ya Jumuiya ya Afrika Mashariki, kwa Sudan Kusini
kuwa mwanachama Jumuiya ya Afrika Mashariki itakuwa na uwezo wa kufanya
biashara katika eneo lenye takribani watu milioni 150.
Kwa upande wake Rais Yoweri Museveni pamoja na kuunga mkono
yaliyosemwa na Rais Magufuli amempongeza kwa kasi yake nzuri aliyoanza
nayo katika uongozi na amesema ni matumaini yake kuwa nchi wanachama wa
Jumuiya ya Afrika Mashariki sasa zitakuwa katika nafasi nzuri ya kwenda
kwa kasi ya Rais Magufuli katika maendeleo.
No comments: