Ads Top

HABARI ZILIZOVUTA HISIA MWAKA 2017 KATIKA MKOA WASHINYANGA

Mbwembwe pamoja na ushangiliaji wa aina yake zilivyotawala katika Uchaguzi  ndani ya Chama cha Mapinduzi Mkoani Shinyanga kwa mwaka 2017
Wahenga walishasema,ukitaka uhondo wa Ngoma ingia ucheze!!!!!!
Hivi ndivyo ilivyokuwa katika uwanja wa siasa ndani ya CCM Mkoani  Shinyanga  ambapo wanachama wa chama hicho walibuni mbinu ya kuhamasisha namna ya kumpata Mwenyekiti wa Chama hicho Mkoani humo ambapo ilikuwa ni burudani tosha kwa watazamaji wa Uchaguzi wakiwemo waandishi wa Habari.
Kabla ya Uchaguzi na hatua ya kutangaza matokeo ya Uchaguzi ndani ya CCM Mkoani shinyanga kuliibuka mbwembwe na ushangiliaji wa aina yake ambao hautakaa usahaulike.
Mmoja wanachama wa Chama cha Mapinduzi waliotia fola kwa mwaka 2017 ni Mheshimiwa Diwani wa Kata ya Kiloleli iliyoko Wilaya ya Kishapu Mkoani Shinyanga Manyama.
Diwani huyo  alijizolea umaarufu baada ya kubuni mbinu ya kupiga kampeni akitumia chupa ya chai (Thermos) ambayo ilikuwa imetundikwa katikamoja ya nguzo na kila aliyekuwa akipita aliitikisa na hata kuibusu kama ishara fulani kuonyesha dira na mwelekeo wa mgombea waliyekuwa wameona ataweza kuivusha CCM katika Uchaguzi 2020.
Mwandishi wa Makala hii alifuatilia nini ilikuwa uhalisia juu ya chupa ya chai iliyokuwa imetundikwa kama mtindo mpya wa upigaji kampeni ambapo kupata ufafanuzi huo mwandishi alimtafuta Diwani wa Kata ya Kiloleli ambaye alikuwa na haya ya kuzungumza.
Mwandishi: Mheshimiwa Diwani naomba kufahamu ni kipi kilichopelekea mtundike chupa ya chai katika moja ya nguzo za hema iliyokuwa ndani ya ukumbi wa kupigia kura.
Diwani: ndugu mwandishi,hii ni mbinu mpya tuliyoibuni baada ya kukutana na kukubaliana namna gani tutaweka ishara kwa ajili ya kusaidia upigaji wa kampeni kwa mtu wetu ambaye tunaamini anazo sifa za kuivusha CCM katika chaguzi zijazo ukiwemo wa 2020.
Mwandishi:Mbinu hii imebuniwa na nani?
Diwani: “Mbinu hii nimeiasisi mimi,si unajua siasa ni ushindani na siasa kwa upande mwingine ni ubunifu? Sisi kama wapiga kura baada ya kukaa na kuwapima wagombea wetu walioomba kupigiwa kura tuliona nani atakisaidia chama kukifikisha pale tunapotaka na hasa kwa kuendana na kasi ya Mheshimiwa Rais yaani HAPA KAZI TU”
Mwandishi: kwa hiyo mlikuwa mnapiga kura mkijua ni wapi na ni nani anayeshinda?
Diwani: Hapana! Kutokana na mfumo wa Demokrasia,kila mtu anayo haki ya kuchagua mtu au kiongozi anayemtaka hivyo baada ya kupiga kampeni nikiwapa wazo langu wanachama kwa ujumla wao,tulikubaliana kuwa kwa wale watakaokuwa tayari kuniunga mkono juu ya maoni na mawazo yangu ishara kubwa ni kufika na kuibusu na kuitikisa chupa hiyo na ndiyo kilichotokea na baada ya kuona watu wengi wakipita na kuibusu na kuitikisa chupa niliona wazo langu limekubalika na jambo hili lilinifanya nielewe kuwa kazi ya hamasa niliyoifanya ilikuwa imezaa matunda!
Kutokana na uchunguzi uliofanywa na mwandishi wa makala hii, Diwani wa Kata ya Kiloleli Manyama ameweza kuwa mwanasiasa wa mwaka 2017 aliyebuni mbinu ya kuweza kupata matokeo ya kile alichokibuni na kushinda kabla ya kutangazwa kwa matokeo jambo ambalo wengi hata wale ambao wanaweza kuhonga ili wapigiwe kura imekuwa vigumu kujua nai kampigia kura na nani hakumpigia kura mpaka baada ya matokeo ndipo wanapokuja kupata matokeo.
Katika Uchaguzi huo uliofanyika Desemba 5, 2017 katika uwanja wa CCM Kambarage Mjini Shinyanga,Mabala Mlolwa aliibuka kidedea baada ya kuwabwaga washindani wake ambapo Mlolwa alipata kura 702  John Festo Makune kura 35 na Cornel Ngudungi  akiambulia kura 02.
Msimamizi wa uchaguzi na mlezi wa Chama hicho Mkoani Shinyanga Abdallah Juma Magodi  ambaye pia ni Naibu Katibu Mkuu Chama Cha Mapinduzi (CCM) Zanzibar alimtangaza Mabala Mlolwa kuwa ndiye mshindi wa nafasi ya Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi Mkoa wa Shinyanga.
“Naomba kusoma matokeo ya kazi tuliyoifanya,Ndugu Mabala Mlolwa kura 702  Ndugu John Festo Makune kura 35 na Cornel Ngudungi kura 02.
“Hivyo kwa mamlaka niliyopewa ya kuwa msimamizi wa Uchaguzi huu namtangaza ndugu Mabala Mlolwa kuwa ndiye Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi Mkoa wa Shinyanga.”alisema Abdallah.
Kwa nafasi ya mjumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa ikichukuliwa na Gaspar Kileo  aliyepata kura 702 dhidi ya wapinzani wake Bernad Shigela aliyepata  kura 33 na
Joyce Masunga-02
.


Diwani wa Kata ya Kiloleli Mh Manyama akiwa na Diwani wa Viti Maalumu pamoja na Mbunge wa Jimbo la Kishapu Mh Suleiman Nchambi mwenye fimbo wakijadili jambo wakiwa na chupa ya chai iliyokuwa ndiyo kivutio cha wajumbe wa Mkutano Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga wakiwa kwenye Uchaguzi wa chama hicho Uwanja wa Kambarage Mkoani Shinyanga. Picha na Antony Sollo.


Wajumbe wakiwa wanaendelea na zoezi la upigaji kura katika ukumbi wa Uwanja wa Kambarage Mkoani Shinyanga.


Mwenyekiti wa  CCM Mkoa wa Shinyanga  Mabala Mlolwa akitoa shukrani kwa wajumbe walimpigia kura baada ya matokeo:  Picha na Antony Sollo



Mjumbe wa NEC Ndugu Gasper Kileo akitoa shukrani baada ya kutangazwa mshindi wa nafasi hiyo: Picha na Antony Sollo

Wajumbe wakiwa wanaendelea na zoezi la upigaji kura katika ukumbi wa Uwanja wa Kambarage Mkoani Shinyanga. Picha na Antony Sollo.


Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Zainab Telak akiwa na msimamizi wa Uchaguzi na mlezi wa Chama cha Mapinduzi Mkoa wa Shinyanga ndugu Abdallah Juma Magodi  ambaye pia ni Naibu Katibu Mkuu Chama Cha Mapinduzi (CCM) Zanzibar Picha na Antony Sollo.


No comments:

UHURUTZ. Theme images by hanoded. Powered by Blogger.