Ads Top

Siku moja baada ya wabunge kuwataka Waziri Mkuu Mizengo Pinda na Waziri wa Maliasili na Utalii, Khamis Kagasheki kujiuzulu kwa kushindwa kusimamia Operesheni Tokomeza Ujangili, pembe 706 za ndovu zimekamatwa jijini Dar es Salaam.

 Waziri wa Maliasili na Utalii, Khamis Kagasheki (wa pili kushoto), akiwa ameshika pembe za ndovu zilizokatwa jana jijini Dar es Salaam toka kwa raia watatu wa China katika operesheni aliyoiongoza.

Pembe hizo 706 ni sawa na tembo 353 waliouawa katika hifadhi za wanyama pori mbalimbali hapa nchini. Tukio hilo lililotokea jana jioni katika Mtaa wa Kifaru, Mikocheni, wilayani Kinondoni, liliongozwa na Waziri Kagasheki ambaye aliambatana na Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Tarish Maimuna.
Waliokamatwa na shehena hiyo ya pembe za ndovu ni raia watatu wa China ambao ni Xu Fujie, Chen Jinzha na Huang Qin wote kutoka mji wa Guandung .
Raia hao wa China wamekuwa wakiishi katika nyumba hiyo kwa miaka mingi wakifanya biashara ya kuingiza nchini vitunguu swaumu kutoka China na kusafirisha nje ya nchi makombe yanayopatikana baharini.
Alipoingia ndani ya nyumba hiyo, Kagasheki ambaye aliambatana na askari polisi na baadhi ya maofisa usalama alishuhudia shehena kubwa ya pembe za ndovu ikiwa imehifadhiwa kwenye viroba vyenye uzito wa kilo 50.
Mbali ya kushuhudia shehena ya pembe hizo, alionyeshwa gari maalumu aina ya Toyota Noah ambalo watuhumiwa hao hulitumia kutoa pembe porini na kuyaingiza jijini Dar es Salaam.
Akizungumza katika eneo la tukio mara baada ya kuwakamata alisema kukamatwa kwa watu hao kunatokana na matokeo ya Operesheni Tokomeza Ujangili ambayo imesitishwa na Serikali juzi baada ya wabunge kuilalamikia.
Waziri Kagasheki alisema kwamba katika harakati za kutaka kuwakamata watuhumiwa hao walitoa Sh30 milioni kwa ajili ya kujaribu kuwahonga askari.
“Walitaka kuwahonga askari ili wasikamatwe,” alisema huku akionyesha noti za fedha hizo.
Alisema wabunge wanaomtaka ajiuzulu kwa madai kwamba Operesheni Tokomeza Ujangili imesababisha mauaji ya watu na mifugo wanapoteza muda kwa kuwa mwenye mamlaka ya kumtoa ni Rais Jakaya Kikwete pekee.
“Sasa mimi nasema kunitoa haitakuwa rahisi anayeweza kunitoa ni yule aliyeniweka,” alisema.
Alisema ipo mikakati inayofanywa na baadhi ya wabunge kutaka kuwang’oa baadhi ya mawaziri kwa masilahi binafsi ya kisiasa.  
GONGA HAPA KWA HABARI ZAIDI

No comments:

UHURUTZ. Theme images by hanoded. Powered by Blogger.