JESHI LA POLISI LAWAKAMATA WALIOKATA KATA MIFUGO YA MFUGAJI WA KIMASAI MVOMERO.
Jeshi la Polisi mkoani Morogoro linawashikilia watu 21 wakiwemo
wenyeviti wa vijiji vya Mkindo, Dihombo na Kambala wilayani Mvomero, kwa
tuhuma za kuwakata mifugo wa mfugaji mmoja wa jamii ya Kimasai, na
mmoja kati yao ambaye ni mfugaji akituhumiwa kulisha mifugo kwenye
shamba la mkulima na kujeruhi.
Akizungumza na waandishi wa habari kuhusu chanzo cha kikundi hicho
cha wakulima kuvamia na kukata kata mifugo, kamanda wa polisi mkoa wa
Morogoro Leonard Paulo, amesema awali mnamo Februari 7 mwaka huu, kundi
la Ng’ombe zaidi ya 50 likiwa na wachungaji watatu wa jamii ya kimasai,
waliingia kwenye shamba la mpunga la hekari moja la Rajab Issa, mkazi
wa Dihombo, ambapo mmiliki wake aliwazuia Ng’ombe hao, lakini
walijitokeza vijana wanaosadikiwa kuwa morani wa kimasai na kuwachukua
ng’ombe hao kwa nguvu, jambo lililofanya mmiliki wa shamba hilo kuripoti
tukio hilo polisi.
Kamanda Paul amesema wakati tukio hilo likishughulikiwa na polisi,
kikundi cha kijadi cha wakulima maarufu kama mwano kilivamia nyumbani
kwa mfugaji wa kimasai, Bi Nuru Keteboi, akiwa nyumbani huku mifugo yake
aina ya mbuzi, kondoo na ndama wakiwa malishoni, na kumpokonya simu ya
mkononi asiweze kuomba msaada, badala yake wakaipeleka mifugo hiyo
porini na kuwakata kata kwa vitu vyenye ncha kali na kusababisha baadhi
yake kufa na wengine kujeruhiwa, na polisi wamewatia mbaroni watu 21
wakiwemo 20 waliohusika na tukio hilo, na mfugaji Kashu Moreto ambaye ni
mwenyekiti wa kijiji cha Kambala kwa tuhuma za kumjeruhi Ramadhani
Juma, huku ikiwasaka wengine zaidi kuhusiana na tukio hilo.
Wenyeviti wengine waliokamatwa ni wa kijiji cha Mkindo Patrick
Longomiza na mwenyekiti wa kijiji cha Dihombo, Christian Thomas
wakituhumiwa kwenye tukio la kukatwa katwa mifugo.
Amewaonya wananchi kuacha kujichukulia sheria mikononi, hususani
vijana akiwaonya kuacha kukubali kutumika kushiriki vurugu au kufanya
matukio ya kiuhalifu, huku akibainisha mgogoro wote unachangiwa na
tatizo la umiliki wa bonde la mgongola ambalo kesi yake bado
inashughulikiwa na mahakama.
Awali kwenye mkutano na waziri wa kilimo, mifugo na uvuvi Mwigulu
Nchemba aliyetembelea kijijini hapo, mtuhumiwa kashu ambaye ni
mwenyekiti wa kijiji cha Kambala, ambaye wananchi walisema hakamatiki
kirahisi, alidai serikali ilishawazuia makundi ya wakulima na wafugaji
kutumia vikundi vya kijadi inapotokea mgogoro wowote lakini
wanashangazwa wakulima kuendelea kutumia vikundi hivyo.
No comments: