RAIS DKT: MAGUFULI ATEMBELEA KWA GHAFLA WODI YA WAZAZI KATIKA HOSPITALI YA TAIFA MUHIMBILI.BOFYA HAPA
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli
ametembelea kwa ghafla wodi ya Wazazi katika Hospitali ya Taifa
Muhimbili Jijini Dar es salaam, na kujionea hali ya msongamano mkubwa wa
wazazi uliosababishwa na uhaba wa vitanda na nafasi finyu katika wodi
hiyo.
Rais Magufuli aliyekuwa akitoka katika Taasisi ya Moyo ya Jakaya
Kikwete alikokwenda kumuona na kumjulia hali Mufti wa Tanzania Sheikh
Abubakar Zubery Bin Ally, amelazimika kwenda katika wodi hiyo baada ya
msafara wake kusimamishwa na kundi la akina mama, waliomtaka kwenda
katika wodi ya wazazi ili akajionee jinsi wazazi wanavyokabiliwa na kero
mbalimbali ikiwemo ya kulala chini kutokana na kukosa vitanda.
Baada ya kujionea mwenyewe kero ya msongamano na kuzungumza baadhi
wazazi waliojifungua, Rais Magufuli amewaahidi wazazi hao kuwa
atashughulikia kero alizozishuhudia.
"Nimeiona hali halisi mimi mwenyewe, watu wanapata shida, watu wana
mateso, na ndio maana nimeamua kuja kwa makusudi, sikuomba ruhusa ili
nijionee hali ilivyo, nimejifunza mengi, ninayabeba na nitajua namna ya
kuyatatua" Alisema Rais Magufuli.
Kabla ya kutembelea wodi ya wazazi, Dkt. Magufuli amemjulia hali
Mufti wa Tanzania Sheikh Abubakar Zubery Ally aliyelazwa katika Taasisi
ya Moyo ya Jakaya Kikwete ambapo amempa pole na kumuombea apone haraka.
Pamoja na kupokea pole ya Rais, Mufti wa Tanzania ameongoza dua ya
kumuombea heri Rais Magufuli ili aweze kutekeleza vyema majukumu yake
katika kuwahudumia watanzania.
Dua kama hiyo pia imefanywa na wananchi wengine waliokuwa
wakimsubiri nje ya majengo ya Hospitali ya Taifa Muhimbili ambapo katika
dua hiyo wamemuomba Mwenyezi Mungu kumlinda na kumuongoza katika
majukumu yake ya kuiongoza nchi.
"Mwenyezi Mungu mbariki Rais wetu, mpe hekima, busara na upendo
katika kazi zake za kuiongoza nchi hii ili watanzania wote wanufaike"
ilisema sehemu ya dua hiyo iliyoongozwa na mmoja wa akina Mama.
No comments: