Wakati Tanzania imejiandaa kupokea ugeni mkubwa kimataifa kwa siku mbili kuanzia leo, kumekuwa na maswali mengi ambayo wananchi pamoja na wachambuzi wa masuala ya siasa za kimataifa wamekuwa wakijiuliza juu ya ujio wa Rais Obama wa Marekani katika ardhi ya Tanzania
Miongoni mwa maswali hayo ni pamoja na anakuja Tanzania kufanya
nini? Kwa nini hatembelei Kenya ambako ndiko hasa asili yake? Pamoja na
wale ambao wamekuwa na wasiwasi juu ya rasilimali za nchi hasa gesi.
Katika mahojiano maalumu na gazeti hili, Waziri wa Mambo ya Nje na
Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe anafafanua zaidi kuhusu ziara
hiyo , umuhimu na manufaa yake.
Urafiki wa Tanzania na Marekani
Waziri Membe anasema nchi hizi mbili zimekuwa na
urafiki wa karibu sana katika kipindi cha muongo mmoja na nusu (miaka
15) ushirikiano baina ya nchi hizi mbili umeongezeka. Anasema urafiki
huo ulianza kuimarika baada ya kulipuliwa kwa ubalozi wa Marekani nchini
mwaka 1998.
Anakumbuka baada ya kutokea mlipuko katika ubalozi
huo jijini Dar es Salaam, Tanzania ilishirikiana kwa karibu na Marekani
katika kuhakisha kwamba watuhumiwa wanasakwa, kukamatwa na kushtakiwa,
huku katika mataifa mengine haikufanyika hivyo.
Anasema kitendo hicho kiliongeza ‘uaminifu’ kwa
Serikali ya Marekani ambayo katika kipindi hicho iliongozwa na Bill
Clinton. Ukarimu wa Watanzania ukaifanya nchi yao ipendwe na utawala wa
George W. Bush na sasa Obama.
Demokrasia na Utawala Bora
Katika hilo, Membe anasema Tanzania kwa kiwango
kikubwa imekuwa inatekeleza misingi ya utawala bora, uhuru wa kupata
habari, haki za binadamu. Anasema hata kama kumekuwa na malalamiko juu
ya suala la utekelezaji wa haki za binadamu na utawala bora nchini bado
Tanzania iko katika nafasi nzuri zaidi katika takwimu kidunia
ukilinganisha na nchi nyingine barani Afrika.
“Ni kweli kwamba tumekuwa tunafanya vizuri katika
kigezo cha demokrasia na utawala bora ukilinganisha na nchi nyingine
Afrika….katika ‘Peace Index’ (kiwango cha Amani) tunashika nafasi ya 53
duniani , Kenya wapo nafasi ya 135, Rwanda 136 na Burundi 144,” anasema
Membe.
Nafasi ya Tanzania Ukanda wa Maziwa Makuu, Kimataifa
Akizungumzia nafasi ya Tanzania katika kutatua
migogoro, Membe anasema nchi imekuwa kinara katika utatuzi wa migogoro
katika nchi jirani, mfano ,Kenya, Zimbabwe, Comoro pamoja na Madagascar
Lakini, pia waziri huyo anasema kwamba msimamo wa Tanzania katika masuala ya kimataifa umekuwa unaeleweka bayana.
“Msimamo wetu kuhusu masuala ya kimataifa umekuwa
unaeleweka bayana tena bila kuyumbishwa na mtu wala taifa
lolote…..msimamo wetu kuhusu Israel na Palestinaunaeleweka siku zote
pamoja na Kosovo.,” anasena.
Akaongeza:“Tanzania ni Mwenyekiti wa Kamati ya
Ulinzi na Usalama wa nchi za kusini mwa Jangwa la Sahara (SADC), lakini
pia ni mjumbe wa Kamati Tendaji ya Jumuiya ya Madola (Commonwealth)
pamoja na hayo tumekuwa mwenyekiti wa Baraza la Ulinzi na Usalama la
Umoja wa Afrika mpaka Aprili mwaka huu.”
‘Power Africa’
Rais Barack Obama anataka kuacha kitu ambacho bara
la Afrika litamkumbuka ‘legacy’ katika kuhakikisha kwamba mbali na kuwa
bara la giza kwa maana ya kukosa nishati ya kutosha. Kuhusu hilo, Membe
anasema lengo la ‘Power Africa’ ni kuhakikisha kwamba bara hili
linazalisha umeme wa kutosha.
Waziri huyo anasema kama kutakuwa na umeme wa
kutosha na sio ule wa kuwasha taa za majumbani, kutakuwa na mabadiliko
makubwa sana ya kiuchumi. Anasema yeye anaamini kwamba umeme ni uchumi,
hivyo kutakuwa na uwezekano mkubwa zaidi wa kuongeza thamani ya mazao
kutoka kwa wakulima na kuyauza kwa bei itakayompatia manufaa mkulima.
“Hii dhana ya Power Africa kwa Tanzania ina maana kubwa sana….tumekuwa
na tatizo kubwa sana la umeme. Ila sasa katika mipango iliyopo kuna kila
dalili kwamba tutaondokewa na tatizo hilo kwa kuzalisha umeme wa
uhakika na wa kutosha,” anasema
Miradi ya MCC
Membe anasema kwamba, Tanzania ni nchi ya pili
baada ya Morocco katika kupokea fedha za akaunti ya changamoto za
milenia kutoka Serikali ya Marekani.
Anasema katika awamu ya kwanza Tanzania ilipokea
dola za Marekani milioni 698 ili kutekeleza miradi ya maendeleo.
Marekani kupitia MCC inagharimia miradi ikiwamo ya maji, umeme na
barabara.
No comments: