Bunge Maalum la Katiba lilivyoendelea na mjadala wa Rasimu ya Katiba Leo Mjini Dodoma
Baadhi ya Wajumbe wa Bunge Maalum la Katiba
wakiingia ndani ya Bunge hilo leo 10 Septemba, 2014 kwa ajili ya kuendelea na
mjadala wa Rasimu ya Katiba.
|
Mwenyekiti wa Bunge Maalum la Katiba, Mhe.
Samuel Sitta akitoa maelezo muhimu wakati wa mjadala wa Bunge hilo leo 10
Septemba, 2014 Bungeni mjini Dodoma.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Balozi Seif
Ali Iddi (wa kwanza kulia) akiwa pamoja na wajumbe wengine wa Bunge Maalum la
Katiba. Kushoto ni Mhe. Pandu Ameir Kificho na katikati ni Mhe. Seif Khatibu.
|
Mzee Kingunge Ngombale Mwiru (kushoto) akiwa na mjumbe wa Bunge Maalum la Katiba,
Mhe. Margareth Sitta wakifuatilia mjadala ndani ya Bunge hilo leo 10
Septemba, 2014 Bungeni mjini Dodoma.
|
Mjumbe wa Bunge Maalum la Katiba toka Kamati
namba Tano, Mhe. Asha-Rose Migiro (kushoto) akiwa pamoja na Mwanasheria Mkuu
wa Serikali Frederick Werema wakifuatilia mjadala wa Bunge hilo 10 Septemba,
2014 Bungeni mjini Dodoma.
|
Mjumbe wa Bunge Maalum la Katiba, Mhe.
Angellah Kairuki (kushoto) akiwa na Mwakilishi wa Watanzania waishio
Marekani, Mhe. Kadari Singo wakifuatilia mjadala ndani ya Bunge hilo leo 10
Septemba, 2014 Bungeni mjini Dodoma.
|
Baadhi ya Wajumbe wa Bunge Maalum la Katiba
wakiendelea kufuatilia mjadala wa Bunge hilo leo 10 Septemba, 2014 Bungeni
mjini Dodoma.Picha zote na Benedict
Liwenga, Dodoma
Na Benedict Liwenga, Dodoma.
BUNGE Maalum la Katiba leotarehe 10 Septemba,
2014 limeendelea na kazi yake ya kusoma na kujadili taarifa za Kamati
mbalimbali Bungeni mjini Dodoma.
Baadhi ya mambo
yaliyojadiliwa katika Bunge hilo ni pamoja masuala ya migogoro ya ardhi
inayowahusisha wafugaji na wakulima, mambo ya Uraia pacha, haki ya afya, haki
ya kuishi ikiwemo sheria ya kunyonga, haki za binadamu, haki ya Mtuhumiwa na
Mfungwa, haki za wafanyakazi na ajira pamoja umri katika ajira pamoja haki za
vijana.
Akizungumza wakati wa
mjadala huo, Mjumbe wa Kamati namba Sita, Mhe. Zaina Madabidaamesema kuwa ni
vema kuwepo kwa kipengele kinachotambua mila na desturi za makundi ya wafugaji
na wakulima ili kuondoa migogoro ya ardhi ambayo imekuwa ikijitokeza mara kwa
mara hapa nchini.
Kuhusu masuala ya Uraia,
Mhe. Madabida ameeleza kuwa si vema kumtambua mtoto mwenye miaka Saba kama raia
Mtanzania aliyekanyaga katika ardhi ya Tanzania na badala yake ni vema mtoto
mchanga ndiyo atambulike kama raia halisi wa Tanzania kikatiba kama Mtanzania,
hivyo yeye na Kamati yake wamekubaliana kumtambua mtoto mchanga kama Mtanzania
halisi ambaye atakuwa amekanyaga katika ardhi ya hiyo.
“Mtoto ambaye ni raia
halisi wa Tanzania atakayekutwa katika ardhi ya Tanzania itambulike kuwa ni
yule mtoto mchanga na sio yule mwenye umri wa miaka Saba”, alisema Mhe.
Madabida.
Aidha, Mhe. Madabida
amegusia suala la Sheria ya Haki ya kuishi pamoja na Sheria ya kunyonga akisema
kuwa Sheria hiyo ya kunyonga ni vema iendelee kuwepo katika Katiba kwani kuna
watu ambao wao wanaua wenzao.
“Adhabu ya kifo iendelee
kuwepo kama Katiba yetu ya sasa inavyosema kwani kuna watu wao wamekuwa
wakiwaua wenzao”, alisema Mhe. Madabida.
Kwa upande mwingine,
mjumbe toka kamati namba Tisa amezungumzia kuhusu suala la haki za binadamu
akitaja Ibara ya 24 katika Sura ya Nne, nae amesema kuwa maoni ya wachache
yamefafanua kuwa haki ya kuishi ianzie tangu pale mimba inapotungwa kwani
sikuhizi watu wengi wamekuwa na utaalamu sana katika kutambua viumbe vilivyopo
tumboni, hivyo watu hao wamekuwa wakikatiza uhai wa viumbe wasiokuwa na hatia.
Mjumbe ameongeza kuwa
katika Ibara ya 39 inayohusu haki ya Mtuhumiwa na Mfungwa, yeye na kamati yake
wameitaka Katiba izingatie mazingira rafiki kwa watuhumiwa wenye ulemavu na
izingatie kuhusu suala la miundombinu kwa walemavu hao ili iwe rafiki kwani
Magereza mengi nchini yalijengwa kipindi kirefu.
Naye mjumbe wa kamati
namba Kumi, Mhe. Monica Sophu amezungumzia kuhusu suala la ardhi akisema kuwa
katika mambo yanayohusiana na masuala ya ardhi, ni vema ikaundwa Tume Huru ya
Ardhi ambayo itakuwa ina kazi ya kushughulikia masuala hayo ili kuepusha
migogoro inayojitokeza baina ya makundi mbalimbali.
“Katika kutatua suala la
migogoro ya ardhi kati ya wakulima na wafugaji, ni vema kukawepo na Tume Huru ya
Ardhi itakayoshughulikia masuala hayo, hivyo Katiba iwatendee haki makundi
haya”, alisema Mhe. Sophu.
Naye mjumbe wa Kundi la
201, Mhe. Jesca Msavatavangu amezungumzia juu ya haki za Vijana nchini akisema
kuwa, haki hizo za vijana hazijaainishwa vema, hivyo ameshauri kuwa ni vema
sasa Katiba ikaainisha vema haki hizo ikiwemo kuelezea juu ya ushiriki wao
katika nafasi za uongozi pamoja na kupewa fursa kushiriki katika mambo ya
kiuchumi.
“Serikali iweke namna ya
kuwaelimisha vijana wetu kuhusu kazi ili wawe na ujasiri na wajengewe uwezo,
pia vijana wapewe fursa ili waweze kushiriki katika nyanja za kiutamaduni,
walindwe dhidi ya afya na uhai wao”, alisema Mhe. Msavatavangu.
Kuhusiana na suala la
Uraia wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Msavatavangu amesema kuwa Sura
ya 56 inayohusu suala la uraia huo ni vema likachukuliwa kwa umakini mkubwa,
aidha ameshauri kuwa ni vema kuwa na uraia wa nchi moja kwani Tanzania bado
haijaweza kujilinda vyakutosha kuweza kukabiliana vitendo viovu vinavyoweza kujitokeza.
“Watu watatumia fursa
hii ya Uraia pacha kuhujumu uchumi wetu, kwani kuna mazingira mengi ya rushwa,
hivyo suala la hili la uraia pacha lije kufikiriwa baadaye sana sio sasahivi”,
alisema Mhe. Msavatavangu.
Naye mjumbe mwingine wa
Bunge hilo, Mhe. Yahya Kassim Issa amegusia kuhusu suala hilo hilo la Uraia
pacha akitaja Ibara ya 38 inayohusu suala la uraia, amesema kuwa kuna watu
wenye watoto wao nje ya nchi na kwa ubinafsi wao ndiyo wanatumia nafasi hiyo kudai
uraia huo badala ya kujali uzalendo na usalama wa nchi yao.
“Haiwezekani kwa mtu uwe
na uraia wa nchi mbili halafu uwe Mwadilifu katika nchi zote hizo mbili”,
alisema Mhe. Issa.
Bunge hilo linaendelea na kazi ya kusoma na kujadili taarifa za kamati mbalimbali kama ilivyopangwa ambapo wajumbe toka kamati husika wanachangia michango toka katika kamati zao kwa lengo la kujadili ndani ya Bunge hilo.
No comments: